ASKARI mmoja wa kampuni binafsi ya ulinzi nchini Kenya, ameburuzwa katika mahakama ya Kibera kwa tuhuma za kumrekodi mwanamke akiwa msalani katika mtaa wa Westlands jijini Nairobi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Nairobi … (endelea)
Askari huyo Mark Mutongoi ambaye ni mlinzi katika kituo cha mafuta cha Rubis kilichoko katika mitaa hiyo ya Westlands, alipandishwa kizimbani jana tarehe 18 Oktoba, 2021 kwa tuhuma za kumrekodi video Margret Wangari bila ridhaa yake.
Askari huyo alimweleza Hakimu Charles Mwaniki kuwa wakati anatenda kosa hilo alikuwa ameingiwa na pepo mbaya.
Akisoma karatasi ya maelezo ya shtaka hilo, Mwendesha mashtaka wa mahakama hiyo, Robert Ogallo amesema askari huyo alimrekodi video Margret Wangari kwa makusudi bila idhini yake.
Alisema alifanya kosa hilo tarehe 7 Oktoba, 2021 katika kituo cha mafuta cha Rubis kilicho katika mtaa wa Westlands.
Akijitetea mbele ya mahakama hiyo, Askari huyo alidai kuwa alimrekodi mwanamke huyo ili kufurahisha macho yake.
Akifafanua kwa kina, Mwendesha mashtaka huyo amesema mlalamikaji yaani Wangari alikuwa amekwenda kuweka gari yake mafuta ndipo alipoamua kuingia msalani kujisaidia.
Alisema baada ya Wangari kumaliza kujisaidia alisikia mtu akitembea nyuma ya choo alichokuwepo na hapo ndipo alipogundua kuwa mshtakiwa alikuwa ameweka simu kwenye dirisha la choo hicho na kumrekodi.
Kutokana na hali hiyo Wangari aliwaeleza wafanyakazi wengine wa kituo hicho waliokuwa pale kuhusu kilichomtokea na ndipo kesi ikaripotiwa polisi na mtuhumiwa kukamatwa.
Mwendesha mashtaka alipendekeza picha za CCTV zitumike kama ushahidi kwenye kesi hiyo lakini Hakimu akaamuru zisitumike.
Aidha, Hakimu huyo aliahirisha kesi hiyo hadi tarehe mosi Novemba mwaka huu.
Leave a comment