RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema mawakili wa Serikali ambao hawatajisajili katika Chama cha Mawakili wa Serikali katika muda utakaotolewa wataondolewa katika nafasi zao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mkuu huyo wa nchi ametoa kauli hiyo leo Alhamisi tarehe 29 Septemba 2022, wakati akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Chama cha Mawakili wa Serikali ambacho pia kitazinduliwa leo.
Amemwagiza Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwahimiza mawakili wa Serikali kujisajili katika chama hicho ambacho ameelezea umuhimu wake karibu na wananchi katika utekelezaji wa majukumu yao.
“Nipongeze hatua ya kuanzisha chama hiki kitakachosaidia kuratibu wanasheria wote walio katika utumishi wa umma nchini,” amesema Rais Samia na kuongeza;
“Kwa wale ambao bado hawajjajisajili basi nihimize tu wajisajili vinginevyo baada ya muda kupita hatutawatambua kama mawakili wa serikali, itabidi watafute sekta ya nje waingie au sijui watepewa kinga gani na wanasheria Mkuu ili waingie tena kama mawakili wa Serikali lakini amri imeshatolewa mawakili mjisajili muda umetolewa kama mtu hajajisajili awe na dharura ya maana sana labda awe hospitali anaumwa hawezi au aliko hakuna mtandao taarifa haikumfikia,” amesema Rais Samia.
Ameeleza majukumu ya chama hicho kupitia mlezi wao ni kuweza kuwasemea masuala yao ya kitaaluma kikazi kinidhamu na kimaslahi na kwamba maboresho hayo yatawaongezea ari na tija katika uetekelezaji wa majukumu yao.
Amesema usajili huo utamsaidia Mwanasheria Mkuu kujua nani ni nani na yupo wapi na kufuatilia utendaji wa mawakili na kumpongeza kwa kuanzisha mfumo wa kielekroniki utakaoweza kufuatilia ugawaji wa kazi za mawakili na kwamba utafanya kazi kama mtandao wa mahakama unavyofanyakazi.
Amesema mfumo huo pia utaonesha kila wakili yupo wapi anafanya kazi gani na kuweka sheria zote za nchi ili kusaidia watakaozihitaji.
Leave a comment