MAWAKILI wa Serikali, wametakiwa kutumia chama chao kuhakikisha viongozi wa Serikali wanazingatia matakwa ya katiba na sheria za nchi, katika utekelezaji wa majukumu yao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Alhamisi, tarehe 29 Septemba 2022, katika hafla ya uzinduzi wa Chama cha Mawakili wa Serikali, uliofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan, jijini Dodoma.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma, amewataka wanasheria hao wa Serikali, wahakikishe sheria zilizotungwa na Bunge, zinatekelezwa kama ilivyokusudiwa.
“Kuna mambo kadhaa niwaombe jukwaa lenu siku za baadae muweze kutafakari. La kwanza haitoshi kuwa na sheria nzuri ambayo haitekelezwi au haitimizi malengo ambayo sheria imetungwa,” amesema Prof. Juma na kuongeza:
“Nadhani siku zote tutafakari, tusitekeleze sheria ambayo pengine tunaona haina matunda tuliyotarajia na wale waliotunga. Tukubali ziko sheria ambazo ni vikwazo kwa maendeleo, baishara na uwekezaji.”
Naye Mwanasheria Mkuu wa Serikali wa zamani, Andrew Chenge, amewataka mawakili hao watumie chama chao kipya kuboreesha sekta ya sheria nchini.
“Limegusiwa suala zima la utawala wa sheria, utawala bora ndiyo msingi wenu ninyi. Hakikisheni utawala wa sheria unatamalaki hapa nchini kupitia chama chenu na sio watawala wa sheria. Kuna tofauti kati ya utawala wa sheria na watawala wa sheria, kazi yenu sasa mawakili wa Serikali ni kuhakikisha viongozi wote wa Serikali na taasisi zake wanazingatia sheria. Tunaposema sheria tunaanza na sheria mama ambayo ni katiba ya nchi na sheria nyingine,” amesema Chenge na kuongeza:
“Kupitia tume ya kurekebisha sheria mnaweza mkayabeba yale ambayo yanahitajika kufanyiwa maboresho katika sheria mbalimbali ambapo ningekuwa na muda ningewasaidia kuwatajia kwamba haya yanawasumbua wananchi wetu.”
Leave a comment