DAMIEN Tarel, amehukumiwa kifungo cha miezi minne jela, kwa kosa la kumpiga kofi Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron, hadharani. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Jana Alhamisi tarehe 10 Juni 2021, Mahakama ya Ufaransa, ilimhukumu Tarel kwenda jela miezi 18, baada ya kumkuta na hatia katika shtaka la shambulio dhidi ya afisa wa umma.
Mwendesha mashtaka wa mahakama hiyo, alitoa hukumu hiyo akisema kitendo kilichofanywa na Tarel hakikubaliki, kwa kuwa ni kitendo cha kuzua ghasia kwa makusudi.
Tukio hilo lililotikisa dunia, lilitokea tarehe 8 Juni 2021, katika ziara ya Rais Macron kwenye Shule ya Hoteli iliyoko kwenye Mji wa Tain-I’Hermitage, mkoani Drom, nje ya Jiji la Valance, nchini Ufaransa.
Rais Macron alikumbwa na kadhia hiyo, wakati akiwasalimia wananchi waliojitokeza katika ziara yake, na kwamba alipofika karibu na Tarel, raia huyo alimpiga kofi la shavuni.
Baada ya kufanya tukio hilo, Tarel aliwekwa kizuizini tangu Jumanne hadi jana, alipohukumiwa kutumikia kifungo cha miezi minne jela.
Hata hivyo, mfungwa huyo anaonekana kutojutia kitendo alichokifanya kwani, alidhamiria kutenda kosa hilo, kabla ya Rais Macron kuzuru katika mkoa huo, akipinga sera zake.
Tarel aliiambia mahakama kwamba, uamuzi wa kumpiga kofi kiongozi huyo wa Ufaransa aliuchukua dakika za mwisho, kwa kuwa awali alipanga kumrushia yai au Ice Cream.
Raia huyo wa Ufaransa aliieleza mahakama hiyo kuwa, Rais Macron anaiharibu nchi hiyo.
Tarel amepunguziwa kifungo hicho, kwani hukumu ya shtaka alilofunguliwa ni miaka mitatu jela na faini ya Euro 45,000.
Leave a comment