RAIS wa Botswana, Mokgweetsi Masisi, amehitimisha ziara ya kikazi ya siku mbili nchini Tanzania na kuondoka kurejea nchini mwake. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea).
Masisi ameondoka leo Ijumaa, tarehe 11 Juni 2021, saa 5 asubuhi, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam-Tanzania, mara baada ya kumaliza ziara hiyo, aliyoianza jana Alhamisi, kwa mwaliko wa Rais Samia Suluhu Hassan.
Katika Uwanja wa Ndege, Rais Masisi, amesindikizwa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Balozi Liberata Mulamula ambaye pia alimpokea alipowasili nchini humo.
Akizungumzia ziara hiyo, Balozi Mulamula amesema, licha ya Botswana kuwa nchi ndogo “lakini ni tajiri katika madini na mifugo na katika ziara hii, tutafungua milango zaidi kwa wawekezaji.”
“Imekuwa ziara fupi, lakini yenye mafanikio sana na amefurahi kukutana na Rais Samia,” amesema
Balozi Mulamula amesema, “Diplomasia ya Uchumi chini ya Rais Samia imeendelea kuimarika. Tufungue milango zaidi na hii ilikuwa ziara ya kiuchumi zaidi na si ya kisiasa.”
Kuhusu maagizo ya Rais Samia ya kuwataka mawaziri na wataalam wa Tanzania na Botswana kufufua kamati ya kudumu ya pamoja (JPC) ambayo haijakutana tangu mwaka 2009, Balozi Mulamula amesema, watalifanyia kazi agizo hilo kwa maslahi mapana ya mataifa hayo.
“Tume ya pamoja inaangalia sekta mbalimbali kama ya biashara, madini, nishati na maeneo mengine mengi, hii ndiyo inaimalisha ushirikiano mkubwa katika kukuza biashara,” amesema Balozi Mulamula
Leave a comment