CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimetangaza baraza lake kivuli la mawaziri litakalobeba majukumu ya kushughulikia changamoto zinazowakabili wananchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Baraza hilo ni la pili kutangazwa, tangu ACT-Wazalendo lilipounda Baraza la kwanza, ikiwa ni hatua ya kuziba pengo la ombwe la wawakilishi wa upinzani bungeni.
Kiongozi wa ACT-Wazalendo, Dorothy Semu, leo tarehe 20 Machi 2024, ametangaza baraza hilo siku chache baada ya chama hicho kufanya uchaguzi wa viongozi wa ngazi za juu.
“Hili ni baraza la pili tangu azimio la Halmashauri Kuu la mwaka 2022, kwa miaka miwili ya utekelezaji wa majukumu yake limekuwa na mchango mkubwa sana kwa chama na wananchi kwa ujumla,” amesema Semu.
Amesema “mathalani kwa miaka miwili yapo mambo ambayo baraza kivuli iliweka nguvu zaidi kuyasemea ni pamoja na masuala ya ardhi; malalamiko mengi tuliyoyapokea katika utendaji wa baraza ni yale yanayohusua masuala ya ardhi; kuondolewa wananchi, migogoro na kero ya kukosekana kwa ushirikishwaji wa wananchi na ufinyu wa ardhi.”
Semu amesema uteuzi wa wajumbe wa Baraza hilo umezingatia usawa wa kijinsia.
“Kwanza kabisa, napenda kuwajulisha kuwa katika uteuzi huu ninaoenda kuutangaza umezingatia uwakilisha wa kitaifa, uwiano wa kijinsia umeimarika zaidi ameteua jumla ya Wasemaji Wanawake (Mawaziri Vivuli Kamili) 13 kati ya wasemaji wote 25 sawa asilimia 52 ya wasemaji wote, aidha vijana wamezidi kuaminiwa idadi ya vijana ni 22 kati ya wajumbe wote wa baraza ambao ni 47, uwiano huu wa vijana ni sawa na asilimia 47,” -Semu.
Miongoni mwa walioteuliwa katika baraza hilo ni, Isihaka Mchinjita, aliyeteuliwa kuwa Waziri Mkuu Kivuli. Idrisa Kweweta, ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu Kiongozi na katika nafasi ya msemaji wa Wizara ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana na Ajira, ameteuliwa Ndolezi Petro kuishika.
Aliyekuwa kiongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, amesema Baraza hilo limeendelea kuimarika Kwa kuwasemea wananchi na matatizo yao.
“Haikuanza kwa kupangwa lakini Naona sasa inajijenga kitaasisi. Tulipoanza utaratibu huu wa Baraza Kivuli @ACTBarazaKivuli kwa kweli hatukuwa na rekodi ya nyuma. Sasa Naona Taasisi imejijenga na kukomaa. Ni coincidence njema sana,” ameandika Zitto katika mtandao wa X, akimjibu mtu aliyehoji kwa nini nafasi ya Waziri Mkuu Kivuli huchukuliwa na Makamu Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Bara.
Leave a comment