SERIKALI ya Urusi iko katika mpango wa kuongeza wanajeshi wake, ili kujihami na vitisho vya kiusalama, kufuatia kupanuka kwa Jumuiya ya Kujihami ya Nchi za Magharibi (NATO). Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Wizara ya Ulinzi ya taifa hilo, imesema Rais wa Urusi, Vladimir Putin, ametia saini amri ya kuongeza idadi ya wanajeshi 170,000 ili kufikia 1,320,000, sawa na ongezeko la asilimia 15.
Mtandao wa BBC Swahili umeripoti kuwa, uamuzi huo unatokana na ongezeko la nchi jirani za Urusi, kujiunga na NATO, ikiwemo Finland iliyojiunga hivi karibuni, baada ya Urusi kuanzisha operesheni ya kijeshi nchini Ukraine, ikipinga uamuzi wake wa kuomba kujiunga na jumuiya hiyo.
Katika taarifa yake, Wizara ya Ulinzi Urusi imedai taifa hilo linakumbwa na vitisho vya kiusalama, kutokana na ongezeko la vikosi vya kijeshi vya NATO, karibu na mpaka wake.
Urusi imekuwa ikipinga majirani zake kujiunga na NATO kwa madai kuwa hatua hiyo inahatarisha usalama wake kwa kuwa ni sawa na kukaribisha miundombinu ya kijeshi ya jumuiya nchini humo.
Leave a comment