KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC), imeishauri Serikali ianzishe Mfuko Maalum wa Uwekezaji kwa ajili ya kusaidia taasisi na mashirika ya umma yenye ukosefu wa mitaji. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 7 Februari 2023 na Mwenyekiti wa PIC, Jerry Silaa, akiwasilisha taarifa ya mwaka ya shughuli zilizotekelezwa na kamati hiyo, kuanzia Februari 2022 hadi Januari 2023.
Silaa amesema kuwa, mfuko huo utasaidia taasisi hizo zenye uhitaji wa haraka wa mitaji kupata kwa ajili ya kutoa huduma pindi zinapohitajika.
“Vilevile, mfuko huu maalum wa uwekezaji utasaidia kipindi kuna muanguko wa kiuchumi au jambo lolote lisiloweza kuzuilika , ambalo linaathiri mtaji wa taasisi au mashirika ya umma. Chanzo cha fedha cha Mfuko huu kinaweza kuwa fedha ambazo hazijadaiwa kutoka mabenki, taasisi za kifedha zisizo za kibenki, taasisi za bima, kampuni za mawasiliano na asilimia 20 ya mapato yasiyo ya kikodi yanayokusanywa na Ofisi ya Msajili wa Hazina,” amesema Silaa.
Silaa ametaja baadhi ya taasisi ambazo kwa sasa zinakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa mitaji, ikiwemo Wakala wa Umeme na Ufundi (TEMESA) na Shirika la Viwango (TBS). Amesema changamoto hiyo imepeleka taasisi hizo kushindwa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kushindwa kuchangia katika mfuko mkuu wa Serikali.
Mbunge huyo wa Ukonga ametaja taasisi nyingine inayokabiliwa na upungufu wa mitaji kuwa ni Shirika la Hifadhi la Taifa (TANAPA), ambalo idadi ya hifadhi inazoziongoza zimeongezeka kutoka 16 hadi 22, bila ya bajeti yake kuongezeka.
Leave a comment