MBUNGE wa Igunga, Nicholas Ngassa ameishukuru Serikali kwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo, chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hasssan kwani imeibua matumaini kwa viongozi na wananchi wa kada zote nchini. Anaripoti Victor Makinda, Tabora… (endelea).
Akizungumza kwenye kilele cha maadhimisho ya miaka 46 ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Igunga, Ngassa, alisema jimbo lake limepewa fedha nyingi za kuteleza miradi mikubwa ya maendeleo hali ambayo imeibua furaha kubwa na matumaini ya kuondokana na kero mbali mbali zilizokuwa zinawakabili wananchi.
Ngassa alisema kuwa miongoni mwa miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na inayoendelea kutelekezwa jimboni humo ni miradi ya maji, afya, barabara, umeme na miradi ya elimu.
“Serikali ya awamu ya sita, imelipatia jimbo la Igunga, Sh bilioni 21 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa maji katika vijiji 15 fedha zilizotokana na fedha za UVIKO – 19. Kwa upande wa miradi ya afya, zahanati sita zimekarabatiwa na kujengwa vituo viwili vya afya vikubwa,” alisema.
Aliongeza kuwa jumla ya Sh milioni 177 zimetolewa jimboni humo kwa ajili ya ujenzi wa wodi ya kujifungulia Mama na Mtoto hospitali ya wilaya ya Igunga, sambamba na ujenzi wa jengo la huduma za wagonjwa mahututi (ICU).
Ngassa alisema jimbo la Igunga limefunguliwa kwa upande wa miundombinu kwani barabara zake nyingi zilikuwa hazipitiki hususani kipindi cha masika ambapo jumla ya shilingi 4 bilion zimepelekwa jimboni hapo kwa ajili ya ujenzi wa miundomini ya barabara ikiwemo madaraja makubwa mawili katika kata ya Mwamashiga na Kinungu.
“Ninaishukuru serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan kulipatia fedha nyingi za maendeleo jimbo la Igunga ambapo miradi mingi imekamilika kwa wakati na mingine inaendelea kutekelezwa hatua ambayo inawafanya wananchi wa jimbo hili kujawa na furaha na kuendelea kuiamini serikali na CCM,” alisema Ngassa.
Katika hatua nyingine, Ngassa alisema utekelezaji wa miradi ya maendeleo jiimboni hapo unapaswa kwenda sambamba na uimarishwaji wa chama CCM kwa kuwa ndio chama dola ambacho kinatekeleza ilani.
“Niliahidi kujenga ofisi za chama katika kata zote 16 jimboni Igunga na leo hii ninakuomba mwenyekiti wa CCM mkoa uzindue ujenzi wa ofisi hizo,” alisema Ngassa.
Akizindua ujenzi wa ofisi hizo, Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Tabora, Hassan Mwakasuvi, alimpongeza mbunge huyo kwa uamuzi wake na kuwataka wananchi wa jimboni hilo kujitoa kusaidiana na mbunge huyo kufanikisha ujenzi wa ofisi hizo ambazo ujenzi wake unakadiriwa kugharimu jumla ya Sh milioni 480.
Leave a comment