JAMII imetakiwa kuendelea kujitokeza kwa wingi kusaidia kundi la wasichana wenye ulemavu taulo za kike ili kuwawezesha kujistili kipindi wanapoingia mzunguko wa hedhi kama wasichana wengine. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ni baada ya kundi hili la wasichana wenye ulemavu kuonekana ni miongoni mwa kundi linalosahaulika katika jamii kusaidiwa taulo za kike kwa asilimia kubwa.
Kaulo hiyo imetolewa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam na Mratibu wa Umoja wa Waandishi wa Habari Wanawake wanaosaidia watu wenye ulemavu ‘Care for Disability’, Penina Malundo walipotoa taulo hizo kwa wanafunzi wa Shule ya Mtoni Maalum.
Penina alisema taulo za kike ni kiungo muhimu kwa mabinti wakiwemo wenye ulemavu katika kujistili pindi wanapoingia katika siku zao za hedhi.
Alisema taulo hizi zitawasaidia watoto hao kuendelea kuhudhuria masomo yao hata kipindi wawapo kwenye hedhi baada ya masaa saba hadi nane wanapotakiwa kubadili kama inavyoshauriwa na watoa huduma.
“Kundi hili ni miongoni mwa makundi yanayosahaurika kusaidiwa kwenye taulo za kike, hivyo jamii inapaswa kuwakumbuka na kujitoa kwao kwa kufanya hivyo itaweza kuwasaidia wanapoingia katika mizunguko wa hedhi kuwa huru darasanai,” alisema
Kwa Upande wake Katibu wa Umoja huo, Janeth Jovin alisema kampeni hiyo walioanza kwa upande wa mkoa wa Dar es Salaam wameweza kutembelea shule mbili za watoto wenye mahitaji maalum.
Alisema tayari wamewafikia watoto zaidi 300 katika Shule ya Msingi Jeshi la Wokovu pamoja na Mtoni Maalum katika kurudisha tabasamu la watoto hao.
“Tunajua hedhi salama inaadhimishwa kila mwezi wa tano ila sisi tunaamini masuala ya hedhi ni endelevu ndiyo maana tunazidi kuomba watu wajitokeze kusaidia kundi hili la watoto wenye ulemavu, “alisema
Naye Mwenyekiti wa Umoja huo, Mary Geofrey alisema umoja huo umeanzishwa kwa lengo la kusaidia jamii hasa kundi la watu wenye ulemavu.
“Mwezi uliopita ulikuwa ni mwezi wa hedhi salama kwa wanawake, umoja wetu umeadhimisha hili kwa kujichangisha kidogo kwa kushirikiana na watu mbalimbali kwa lengo la kupata taulo za kike za kusaidia wasichana hao wenye ulemavu,” alisema na kuongeza
“Tumeamua kujikita katika kundi hili, kwa sababu tumeona jamii ikijikita kusaidia wasichana waliopo mashuleni ambao ni wazima ila sisi tumeamua kujikita kwa wasichana wenye ulemavu hivyo tumetoa elimu juu ya matumizi ya taulo hizo na namna ya kuzihifadhi baada ya kutumia,” alisema
Aidha, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mtoni Maalum, Nyamisango Mtaki alishukuru umoja huo kwa namna ya walivyojitoa na kukumbuka kundi hilo.
“Tunawashukuru sana kuja kuwafundisha watoto wetu wapate uelewa wa Mambo ya hedhi salama na kujua namna ya kujistili katika siku zao,” alisema.
Leave a comment