CHAMA cha Waajiri Tanzania (ATE) kimesema mrundikano wa kodi zinazotozwa na taasisi mbalimbali za Serikali, umesababisha waajiri kupunguza wafanyakazi. Anaripoti Mwandishi Wetu… (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 1 Mei, 2022 Mwenyekiti ATE, Jayne Nyimbo katika maadhimisho ya siku ya Wafanyakazi Duniani yaliyofanyika jijini Dodoma.
Pia katika maadhimishi hayo ambayo mgeni rasmi ni Rais Samia Suluhu Hassan, Nyimbo ametoa wito kwa waajiri kutopa fursa kwa wahitimu kujifunza kwa vitendo ili kupunguza changamoto ya uzoefu kazini.
“Waajiri tunakabiliwa na changamoto nyingi hasusani katika masuala ya mrundikano wa kodi tunazotozwa na mamlaka mbalimbali hali inayoongeza gharama za kufanya biashara na ugumu wa mazingira ya kufanya biashara.
“Baadhi ya waajiri hujikuta wakilazimika kupunguza wafanyakazi hasa kwenye sekta zilizoathiriwa na janga la Ukimwi na Uviko – 19, mathalani sekta ya utalii na ukarimu,” amesema Mwenyekiti huyo.
Aidha, Nyimo ametoa wito kwa waajiri na wafanyakazi kuendelea kushirikiana na serikali kujenga uchumi, kufanya kazi kwa bidii na kulipa kodi stahiki.
“ATE ambaye ni mwakilishi wa waajiri kutoka sekta binafsi tunaendelea kuwa sauti ya waajiri nchini na kufanya ushirikiano wa Serikali na vyama vya wafanyakazi ni ombi letu kwa wadau wa utatu kuendelea kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja ili kutatua changamoto katika sekta hii maana umoja ni nguvu,” amesema na kuongeza.
“Ombi letu kwako pia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu kutupatia kiwanja kimoja hapa Dodoma ili ATE tuondokane na gharama za kupanga hapa Dodoma,” amesema.
Leave a comment