Sunday , 5 May 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Kina Mbowe wapinga hati ya ukamataji mali
Habari za Siasa

Kina Mbowe wapinga hati ya ukamataji mali

Spread the love

 

MAWAKILI wa utetezi, katika kesi ya ugaidi, inayomkabili Mwenyeketi wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake watatu, wamepinga kupokelewa kwa hati ya ukamataji mali zinazodaiwa kuwa za mshtakiwa, Halfan Bwire Hassan, kwa madai haina uwezo kisheria. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).

Mpaingamizi hayo yametolewa leo Jumatano, tarehe 15 Desemba 2021, mahakamani hapo mbele ya Jaji Joachim Tiganga, baada ya shahidi wa nane wa Jamhuri, Mkuu wa Upelelezi wilayani Arumeru, Arusha, Jumanne Malangahe, kuiomba iipokee kama sehemu ya ushahidi wake.

Baada ya kutoa ombi hilo, wakili wa Hassan, Nashon Kungu, aliweka mapingamizi dhidi ya kupokelewa kwa hati hiyo, akidai shahidi huyo hakueleza kwa nini hati hiyo ina taarifa tofauti ambazo mshtakiwa na mashahidi hawakuzisaini.

“Kwa niaba ya mshtakiwa wa kwanza nina pingamizi, tuna object nyaraka hii kwa kuwa tunaona sio ya ukaguzi na haijashuhudiwa aidha na mashahidi na ushahidi na pamoja na mtuhumiwa mwenyewe, tunaongelea hasa kurasa nyingine hazijazungumziwa, tunaona nyaraka imeongezewa vitu ambavyo havijashuhudiwa na havijaelezwa,” amedai Nkungu na kuongeza:

“Nasemanyaraka hii ina kurasa mbili, kurasa ya kwanza na nyingine imeingizwa kinyemela, haijaelezewa wala haina saini ya shahidi wala ya mshtakiwa mwenyewe. Ndiyo kwa sababau fact hizi hazikuelezwa nyaraka hii, haikuelezwa jinsi zilivyo tunaona ina nyongeza ya maelezo kwa kuwa haijaelezwa tunapinga nyaraka.”

Naye Wakili John Mallya, amepinga upokelewaji wa nyaraka hiyo akidai kwamba, haina uhusiano na haina uwezo, kwa kuwa zoezi lake lilifanyika kwa sheria ambayo haipo.

“Muhimu zaidi imechukuliwa chini ya kifungu cha 31 (1) na (3) cha Sheria ya Makosa ya Mtandao na hiyo utaiona hapa juu, sheria ya makosa ya mtandoa inayozungumza kukamata mtu inasema polisi akamate vitu vinavyohusiana na mifumo ya kompyuta kama simu na kamera lakini mmekamata vifaa vya kijeshi begi la mgongoni na bakuli la kijeshi,” amedai Mallya.

Mallya amedai “zoezi hilo lilikuwa batili haliwezi kuhalalishwa na maombi ya shahidi ya kutaka uipokee nyaraka hiyo kama kielelezo.”

Wakili Mallya amedai, nyaraka hiyo haina uwezo wa kupokelewa kisheria kwa kuwa imehaririwa kinyume cha sheria, “na mheshimiwa jaji, mahakama yako kama ni duka basi hii ni fedha bandia.”

“Nyaraka imekuwa edited, imehaririwa kwa macho yangu nafikiri amehariri shahidi huyo huyo baada ya mashahidi wameshashuhudia, walichokamata namba moja hadi nane, akaenda peke yake akaongeza namba tisa inaanza na mkanda wa JWTZ, akaongeza vingine vingi mpaka namba 19 halafu akasaini peke yake,” amedai Wakili Mallya na kuongeza:

“Kwa mujibu hiki alichoonesha shahidi haijulikani alisaini wapi wala tarehe gani, aidha akaongeza ya kwake akasaini peke yake, hakuna tarehe wala hakuna sahihi ya mashahidi walioshuhudia hichi ambacho amekiongeza yeye peke yake.”

Kwa upande wake Wakili Fredrick Kihweli, amedai shahidi hajaonesha mlolongo wa utunzwaji kielelezo hicho hadi kilipomfikia mahakamani hapo (Chain of Custody), wakati anatoa ushahidi.

Kiongozi wa Jopo la Mawakili wa Utetezi, Peter Kibatala, amedai shahidi huyo hajaithibitisha nyaraka hiyo kama ndiyo aliyoandika baada ya kumfanyia upekuzi Hassan.

“Shahidi hajaongozwa kusema ana uhakika gani kule ilipokuwa ilikuwa katika hali hiyo hiyo aliyoikabidhi na hakuna mazingira yoyote ya maboresho yaliyofanyika na mengineyo,” amedai Kibatala.

Kufuatia mapingamizi hayo, Jaji Tiganga ameahirisha kesi hiyo kwa muda, itakaporejea mawakili jamhuri watazijibu hoja za mapingamizi hayo.

Awali, SP Malangahe alidai kuwa, hati hiyo ya ukamataji mali aliiandaa tarehe 10 Agosti 2020, baada ya kupekua nyumbani kwa Hassan, maeneo ya Yombo Kilakala.

Shahidi huyo wa Jamhuri alidai, katika upekuzi huo, Hassan alikutwa na baadhi ya vifaa na sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Jeshi la Kujenga Taifa.

Kwa mujibu wa SP Malangahe, ukaguzi huo ulifanyika baada ya Hassan kukamatwa maeneo ya Kituo cha Polisi Chang’ombe, Temeke jijini Dar es Salaam, tarehe 9 Agosti mwaka jana, kwa kosa la kula njama za kufanya vitendo vya ugaidi.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

Mbatia ambwaga Selasini, mahakama yaamuru alipwe fidia

Spread the loveMAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, imemuamuru...

Habari za SiasaTangulizi

Mkulo afariki dunia, kuzikwa kesho Kilosa

Spread the loveALIYEKUWA Waziri wa Fedha na Mbunge wa Kilosa (CCM), Mustafa...

Habari za SiasaTangulizi

Sabaya afutiwa kesi, ruksa kugombea uongozi

Spread the loveMwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali DPP leo Ijumaa amefuta rufaa...

Habari za Siasa

Serikali yasaka bilioni 3 kujenga daraja Mto Mpiji

Spread the loveSerikali imesema inaendelea na juhudi za kutafuta fedha kiasi cha...

error: Content is protected !!