Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Kesi ya Mbowe: Polisi aeleza vifaa za JWTZ, JKT vilivyokutwa kwa mstakiwa
Habari za SiasaTangulizi

Kesi ya Mbowe: Polisi aeleza vifaa za JWTZ, JKT vilivyokutwa kwa mstakiwa

Spread the love

 

MKUU wa Upelelezi Wilayani Arumeru, mkoani Arusha, SP Jumanne Malangahe, ameieleza Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, vitu alivyovipata wakati anakagua makazi ya Halfan Bwire Hassan, mshtakiwa wa kwanza, katika kesi ya ugaidi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).

Ni katika kesi ya ugaidi inayowakabili washtakiwa wanne wakiwemo, Bwire na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.

Washtakiwa wengine; ni Adam Kasekwa na Mlhammed Abdillah Ling’wenya.

Malangahe ameeleza vitu hivyo leo Jumatano, tarehe 15 Desemba 2021, akiongizwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Robert Kidando, kutoa ushahidi wake mahakamani hapo mbele ya Jaji Joachim Tiganga.

Malangahe amedai, baada ya Hassan kukamatwa maeneo ya Kituo cha Polisi Chang’ombe, Temeke mkoani Dar es Salaam, tarehe 9 Agosti 2020, walibaini kwamba ana makazi mengine maeneo ya Yombo Kilakala mkoani humo, ambayo mtuhumiwa huyo awali aliyaficha.

Amedai, kesho yake tarehe 10 Agosti 2020, kiongozi wao aliyemtaja kwa jina la ACP Ramadhan Kingai,  pamoja na askari wenzie, walikwenda maeneo hayo kwa ajili ya kufanya taratibu za upekuzi.

Malangahe amedai, baada ya kufika katika eneo hilo, ACP Kingai alimpa maelekezo ya kwenda kufanya upekuzi, zoezi lililoshuhudiwa na kiongozi wa Serikali ya Mtaa husika, mke wa mtuhumiwa aliyemtaja kwa jina la Tumaini John Chacha, mwenye nyumba wa mtuhumiwa huyo, Mariam Abdallah  na mashahidi wengine.

Shahidi huyo wa nane wa Jamhuri amedai, baada ya kufanya upekuzi chumbani kwa mtuhumiwa huyo, alikuta baadhi ya vifaa vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), pamoja na makaratasi aliyodai kuwa na ramani za maeneo ya vituo vya mafuta na masoko ambayo yalipangwa kulipuliwa na mtuhumiwa huyo akishirikiana na wenzake.

Katika kesi hiyo yenye mashtaka sita ya ugaidi, Hassan anatuhumiwa kukutwa na sare za jeshi kinyume cha sheria.

Mahojiano yao yalikuwa kama ifuatavyo;

Shahidi: Tulianza kupekuwa (chumba cha kulala mtuhumiwa) kwenye kile chumba maeneo mbalimbali, kwenye dressing table, mabegi, lakini pia nilipekuwa kwenye kitanda na nilipofika eneo la kitanda kilichokuwa kimeelekea upande wa kaskazini kimepakana na sitting room.

Kidando: Baada ya kuwa umeuona mfuko huo nini kiliendelea?

Shahidi: Nilimalizia kutoa chaga ili nione mfumo una nini, kuna nini uvunguni

Kidando: Baada ya kutoa ulifanya nini?

Shahidi: Baada ya kutoa chaga nilifunua mfuko kuangalia nilichokiona juu nilianza kuona  sare ya Jeshi kombati iko juu.

Baada ya kuona hivyo niliingiza mkono na kuinua nikaona shati ambalo ni kombati kwa ufahamu wangu niliona ni sare ya JWTZ,  baada ya kutoa nikamuuliza mtuhumwia hii vipi? hakunijibu chochote.

Kwa hiyo nilianza kuangalia vitu vilivyomo kujua kuna  vitu gani viko kwenye mfuko kwa kuvitoa vyote

Kidando: Baada ya kutoa vitu, vitu gani ulikuta?

Shahidi: Vitu nilivyokuta kwenye mfuko nilikuta kuna mashati ya JWTZ

Kidando: Yalikuwa ni mangapi?

Shahidi: Kwa kumbukumbu zangu yalikuwa matatu, shati moja la JKT, kulikuwa na mashati mawili ya kombati, kulikuwa na suruali tatu za JWTZ, kulikuwa na suruali moja ya JKT.

Kidando: Kingine uliona nini?

Shahidi: Nikaona michoro ya kulipua mafuta masoko, michoyo imeandikwa BP, Puma na sokoni

Kidando: Baada ya kuviona vitu ulifanyaje?

Shahidi: Niliviorodhesha kwenye hiyo hati ya ukamataji mali

Kidando: Wakati gani uliorodhesha?

Shahidi: Baada ya pale kumaliza kutambua na kukagua, nilianza kujaza hati ya kukamata mali mbele ya mshahidi kama nilivyotaja hapo awali. Baada ya kujaza hati nilimpa mtuhukiwa asaini na kuweka sole gumba,  niliwapa mashahidi wasaini.

Kidando: Baada ya hapo vielelezo hivyo ulivipeleka wapi?

Shahidi: Kituo cha Polisi Kati Dar es Salaam na kuvikabidhi kwa mtunza vilelezo Sergent John.

Shahidi huyo anaendelea kutoa ushahidi wake.

Endelea kufuatilia MwanaHALISI TV, MwanaHALISI Online na mitandao yetu ya kijamii kwa habari na taarifa mbalimbali

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

BiasharaHabari za Siasa

Mavunde aagiza Perseus kuharakisha fidia Sengerema

Spread the loveWaziri wa Madini, Anthony Mavunde ameipongeza Kampuni ya Perseus kwa...

Habari za Siasa

Kigogo Chadema awanyooshea vidole vigogo serikalini kuhusu ripoti ya CAG

Spread the love  MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na...

Habari za Siasa

Wabunge waikalia kooni TAKUKURU Bungeni

Spread the love  BAADHI ya wabunge wamelia na changamoto za utendaji wa...

Habari za SiasaTangulizi

Mpina ataka Waziri Majaliwa ajiuzulu, akosoa teuzi za mawaziri

Spread the love  MBUNGE wa Kisesa, Luhaga Mpina, amemtaka Waziri Mkuu, Kassim...

error: Content is protected !!