MWENYEKITI wa bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere nchini Tanzania, Stephen Wasira amewataka wahitimu wa chuo hicho kuangalia fursa zitakazowasaidia katika maisha yao na Taifa kwa ujumla kupitia mazingira yao ya kila siku. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza kwenye mahafali ya 16 ya chuo hicho yaliyofanyika katika Kampasi ya Kivukoni jijini Dar es Salaam, Wasira amesema kutokana na changamoto za ajira zinazolikabili taifa ipo haja kwa wasomi kutumia elimu waliyoipata kuangalia fursa zinazowazunguka ili waweze kujiajiri.
Zaidi ya wahitimu 4,000 wametunukiwa Astashada ya awali, Astashahada, Stashahada na Shahada.
Wasira amesema kabla ya miaka 60 ya Uhuru nchi ilikuwa haina wasomi wengi kama ilivyo sasa, hivyo watumie mazingira hayo kuangalia fursa zilizopo ili waweze kujiajiri.
Kwa upande wake, Mkuu wa chuo hicho, Prof. Shadrack Mwakalila amesema chuo kimefanikiwa kutekeleza malengo yake ikiwa ni pamoja na kuboresha miundombinu ya hosteli za wanafunzi, madarasa pamoja na ofisi za wafanyakazi ikiwa ni pamoja na kuweka umeme jua kwenye hostel za wanafunzi na barabara.
Pia, chuo kimefanikiwa kuboresha mfumo wa maji taka.
Prof. Mwakalila amesema mshauri elekezi kwa ajili ya ujenzi wa maktaba yenye uwezo wa watu zaidi ya 1500 pamoja na ukumbi wa mihadhara wenye uwezo wa watu 1000 amekamilisha michoro yote na mchakato wa kumpata Mkandarasi kwa ajili ya ujenzi unaendelea.
Mkuu huyo amesema, katika kampasi ya Karume kazi ya ujenzi wa hosteli yenye uwezo wa kulaza wanafunzi 1536 unaendelea vizuri, kwa mujibu wa mkataba ujenzi unatakiwa kukamilika tarehe 22 Desemba 2022.
Aidha, mshauri elekezi ameshakamilisha michoro kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za wafanyakazi 30 na mchakato wa kupata mkandarasi kwa ajili nyumba hizo unaendelea.
Mwakakila amesema chuo kimefanikiwa kuongeza udahili kutoka wanafunzi 9,754 mwaka 2019/2020 hadi 10,032 mwaka 2020/2022.
Pia, katika Kampasi ya Karume – Zanzibar udahili umeongezeka kutoka wanafunzi 1,659 mwaka 2019/2020 hadi 2161 mwaka 2020/2021 na Tawi la Pemba limekuwa na wanafunzi 125 katika mwaka 2020/21 hivyo idadi ya Wanafunzi kwa ujumla hivi sasa ni 12,318.
Aidha amesema, sera ya uthibiti ubora imehuishwa ili kuwezesha mafunzo yanayotolewa kuwa bora na yenye viwango vinavyokubalika Kitafa na Kimataifa.
“Zoezi la kuandaa mitaala mipya na kuhuisha mitaala ya zamani linaendelea ili kuwa na mitaala inayozingatia mahitaji halisi ya kitaifa na kimataifa,” amesema
“Chuo pia kimetenga bajeti kwa ajili ya kuwawezesha Wahadhiri kufanya tafiti mbalimbali zenye maslahi kwa Chuo na Taifa,” amesema Prof. Mwakalia.
Leave a comment