WAZIRI wa Maji nchini Tanzania, Jumaa Aweso amekagua mtambo mkubwa wa kuchuja maji chumvi katika eneo la Serengeti, Wilaya ya Gairo mkoani Morogoro ili kujiridhisha na huduma ya majisafi inayotolewa kwa wananchi. Anaripoti Danson Kaijage…(endelea).
Aweso amefanya ziara hiyo ya kikazi leo Jumamosi, tarehe 4 Septemba 2021 kwa lengo kuu ikiwa ni kuboresha hali ya upatikanaji wa majisafi na salama wilayani Gairo.
Amewataka watalaamu kufanya kazi ya utafiti na kuchimba visima virefu eneo la Ngiloli ili kuongeza haraka iwezekanavyo kiasi cha majisafi kwa wananchi mjini Gairo.
Aidha ameagiza tathmini na hatua za awali zifanyike ili kuweza kutoa maji kutoka chanzo cha maji cha Chagongwe kupeleka mjini Gairo ikiwa ni mpango wa kudumu utakaomaliza changamoto ya uhaba wa huduma ya majisafi.
Waziri Aweso amesema, pamoja na hatua hizo alizoelekeza, amewataka Mamlaka ya Nishati na Maji (Ewura) kufanya kazi ya tathmini ya bei ya majisafi inayotumika mjini Gairo endapo inaendana na uhalisia wa gharama za uendeshaji ili wananchi wasiumie katika kupata huduma ya majisafi.
Leave a comment