RAIS wa Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi amesema katika siku 100 za uongozi wake, amefanikiwa kuimarisha umoja wa Wazanzibari na kuongeza ukusanyaji mapato. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mwanasiasa huyo aliyeapishwa tarehe 2 Novemba 2020 kuiongoza Serikali ya Awamu ya Nane ya Mapinduzi Zanzibar, ameteja mafanikio hayo leo Jumanne, wakati akizungumza na wanahabari visiwani humo.
“Kama mkiniuliza nini mafanikio yako tangu kuingia madarakani, ni kufanikiwa kwetu kuleta umoja wa wananchi na kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa. Nahesabu kama ndio fanikio la kwanza katika utendaji wa serikali ya awamu ya nane,” amesema Rais Mwinyi.
Mwenyekiti huyo wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, amesema kilichoifanya Serikali yake kufanikiwa katika hilo, ni maridhiano aliyofanya na Chama cha ACT-Wazalendo kwa ajili ya kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK).
“Nataka nichukue fursa hii niwashukuru wenzetu kwa kukubali kufanya mazungumzo nasi ambayo yamepelekea kufapata SUK, nashukuru sababu niliona bila ya SUK tungepata shida kuleta maendeleo sababu mazingira yangetusumbua.
Lakini kutokana na maridhiano hayo tumefanikiwa mambo matatu, tumekidhi matakwa ya Katiba ya Zanzibar inayotaka SUK iundwe, tumeleta umoja wananchi wetu. Yale malumbano na chuki zilizokuwepo tunaona kabisa kwa kiwango kikubwa zimepotea,” amesema Rais Mwinyi.
Rais Mwinyi amesema kwa sasa chuki baina ya wananchi imepungua na kwamba Wazanzibar wameacha kurumbana kuhusu masuala ya kisiasa, na sasa wameungana kuleta maendeleo.
Rais Mwinyi amesema katika siku 100 za uongozi wake, amefanikiwa kuongeza kasi ya ukusanyaji mapato, ambapo yamepanda kwa asilimia 49 kutoka Sh. 55 Bil. zilizokusanywa Oktoba hadi Bil. 101 zilizokusanywa Disemba 2020.
“Tumefanikiwa kuongeza ukusanyaji mapato, siku 100 za kwanza mapato yameongezeka sana, mfano Disemba 2020 jumla ya Sh. 101 Bil. zilikusanywa sawa na asilimia 109 ya madirikio ya ukusanyaji wa Sh. 93 Bil. kwa mwezi huo,” amesema Rais Mwinyi.
Rais Mwinyi ameahidi kubana mianya ya upotevu wa mapato, ili kuhakilisha serikali yake inapata fedha za kutosha kujiendesha na kuwahudumia wananchi.
Leave a comment