HALIMA Mdee, mbunge asiye na chama bungeni, amekosoa Mpango wa Maendeleo wa Serikali, kwamba ‘hakuna kitu.’ Anaripoti Mwandshi Wetu, Dodoma…(endelea).
Akichangia mpango huo tarehe 9 Februari 2021, Mdee ambaye alifukuzwa Chadema kwa tuhuma za usaliti amesema, mpango huo hautekelezeki.
Ameeleza kushangazwa na wabunge kuufurahia mpango huo huku akisisitiza, hauna jipya katika kukuza uchumi wa nchi.
“Ukuaji wa uchumi hamna kitu, uwiano wa pato la mtu hakuna kitu, kiwango cha umasikini ni kikubwa. Hapa shida ni wataalamu wetu halafu ninyi mnacheka na kushangilia,” amesema Mdee.
Amefafanua kwamba kuna shida kwa upande wa watalaam wa serikali, huku akipendekeza serikali kujikita zaidi kuwekeza kwenye kilimo kwa maslahi ya Watanzania wengi.
Mdee alieleza kushangazwa na wabunge kuusifu mpango huo huku ukiwa huna jipya na kwamba kuna mabadiliko machache tu.
Mchango huo wa Mdee ulimsukuma Jenister Mhagama, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Ajira na Watu Wenye Ulemavu ambaye mara mbili aliomba kumpa taarifa Mdee kupinga kile alichokuwa akieleza.
Akijibu hoja ya Mdee kwamba ‘hakuna kitu,’ Mhagama amesema, vitu alivyokuwa akizungumza Mdee, serikali imevifanya.
Waziri huyo alisisitiza, kwamba mchangiaji (Mdee) hakuwa na sababu ya kuzungumza yale aliyokuwa akizungumza kwa kuwa yalikuwa yamefanyiwa kazi na serikali.
Leave a comment