MGOMBEA Urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais John Pombe Magufuli amezungumzia madai ya Serikali kutafuna fedha zilizochangwa na wahisani kwa ajili ya waathirika wa tetemeko la ardhi lililotokea mkoani Kagera, tarehe 10 Septemba 2016. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kagera … (endelea).
Rais Magufuli amewataka wananchi wa Bukoba wakisikia watu wanaibua madai hayo, wawapeleke katika maeneo ambayo Serikali imejenga shule kwa kutumia fedha hizo.
Mgombea huyo wa Urais alisema hayo wakati akizungumza katika mkutano wa kampeni za urais za CCM jana Jumatano tarehe 16 Septemba 2020 wilayani Bukoba mkoa wa Kagera.
“Leo ukienda kwenye shule hizo utafikiri umetembelea chuo kikuu, nasema uongo ndugu zangu? Halafu anatokea mtu anasema hela za tetemeko zililiwa na serikali, siku nyingine akija mumpeleke kwenye shule hizo akashangae,” alisema Rais Magufuli.
Tetemeko hilo lilikuwa na ukubwa wa kipimo cha richa 5.9 liliathiri zaidi mkoa wa Kagera, ambapo liliuwa watu zaidi ya 15 huku 170 wakijeruhiwa. Lilibomoa majengo zaidi 800 ikiwemo makanisa na shule.
Kufuatia janga hilo, taasisi za serikali, binafsi na baadhi ya wananchi walichanga fedha kwa ajili ya kupoza machungu walioguswa na athari za tetemeko hilo.
Wakati huo huo, Rais Magufuli alisema, Serikali yake imetekeleza miradi mingi ya maendeleo, hususan katika sekta ya elimu, kwakujenga shule mpya za msingi 27, shule za sekondari 28, shule za kidato cha tano na sita tano.
Pia, imejenga madarasa 1,119, nyumba za walimu 286, imeajiri walimu wapya 1,658 pamoja na kutoa kiasi cha Sh. 57.23 bilioni kwa ajili ta kugharamia elimu bure mkoani humo.
“Kwenye upande wa elimu ndugu zangu wananchi wa Bukoba, shule mpya za msingi 27, za sekondari 28, za kidato cha tano na sita tano mpya zimejenga, aidha tulileta takribani Sh.57.23 bilioni kwa ajili ya kugharamia elimu bila malipo katika mkoa huu,” alisema Rais Magufuli.
Leave a comment