MCHUNGAJI Peter Msigwa, aliyekuwa Mbunge wa Iringa Mjini amesema, hana imani na baadhi ya watendaji wa uchaguzi kuelekea uchaguzi mkuu wa tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Iringa … (endelea).
Na kwamba, tayari amemwandikia barua Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Iringa Mjini kufikisha kilio hicho kuwa, ukada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa watendaji katika zoezi la uchukuaji fomu, umechipua.
Ametoa kauli hiyo leo tarehe 12 Agosti 2020, muda mfupi baada ya kuchukua fomu ya kugombea ubunge wa jimbo hilo, akisisitiza yeye na chama chake watatii sheria lakini si pale itakapovunjwa na kuporwa haki yao.
Amesema, sasa wanaelekea kwenye maeneo mengine ili kuchukua fomu za udiwani huku akionya kwamba, hawako tayari kuchezewa mchezo mchafu.
“Tumemwandikia barua mkurugenzi kwamba kuna baadhi ya wasimamizi, hatuna imani nao na watendaji wengine kama watatu hatuna imani nao, kwa sababu wao wameonesha kabisa ukada wa Chama Cha Mapinduzi.
“Kwa hiyo tungetaka watu wengine ambao wata-playe fair game (watasimama kati) ili tuwe na imani nao…., ,” amesema Mch. Msigwa.
Amesema, yeye na chama chake wapo tayari kufuata maelekezo ya Tume ya Uchaguzi (NEC), ambapo ameahidi kufanya kampeni za haki pamoja na kujilinda.
“Tutatii maelekezo na utaratibu laini hatutakubali pale haki yetu itaingiliwa. Tumejipanga vizuri kama chama na tutaenda kufanya kampeni ya ustarabu japokuwa kijilinda ni haki yetu ya msingi,” amesema.
“Tunaamini figisu nyingi zitafanywa lakini sisi tungependa uchaguzi uwe huru na haki kwa sababu tunaipenda nchi yetu,” amesema.
Leave a comment