LICHA ya ripoti ya maambukizi ya virisi vinavyosababisha ugonjwa wa corona kupungua nchini, ugonjwa huo haujaisha nchini. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya leo tarehe 1 Juni 2020, jijini Tanga wakati wa ufunguzi wa jengo la ofisi za Makao Makuu ya Bodi ya Mkonge Tanzania.
“Tunamshukuru Mungu hali ni nzuri, Tanga hatuna mgonjwa wa corona, kituo kilichokuwa kinatumika kwa wagonjwa wa corona kimefungwa.
“Amana tuna wagonjwa watatu, Mloganzila mmoja, Mwanza hakuna mgonjwa. Tunamshukuru Mungu, hata hivyo corona ipo, tuendelee kuchukua tahadhari kujikinga,” amesema Waziri Ummy.
Amesema, Tanzania imefanikiwa katika kudhibiti kasi ya maambukizi ya ugonjwa huo “corona tumeishinda Tanzania, ukiangalia wenzetu, unajiuliza hivi Tanzania tuna nini? asante Mwenyezi Mungu kwa kutuokoa,” amesema Waziri Ummy.
Mara ya kwanza Tanzania iliripoti kisa chake cha kwanza cha ugonjwa wa Covid-19, tarehe 16 Machi 2020, ambapo siku moja baadae ilitangaza kufunga baadhi ya shughuli zenye mikusanyiko ya watu wengi, ili kudhibiti maambukizi ya ugonjwa huo.
Miongoni mwa shughuli zilizofungwa tarehe 17 na 18 Machi 2020 ni, michezo, shule na vyuo vya kati na vikuu, pamoja na shughuli za kijamii.
Lakini Mei mwaka huu, Rais John Magufuli alitangaza kufunguliwa kwa vyuo pamoja na shughuli za michezo.
Wakati akitangaza kufunguliwa kwa shughuli hizo, Rais Magufuli alisema hatua hiyo imechukuliwa baada ya maambukizi ya Covid-19, kupungua kwa kasi.
Leave a comment