WIZARA ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeitaka Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) kufanya utafiti kuhusu ugonjwa wa Corona (Covid-19). Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Agizo hilo limetolewa leo na Naibu Waziri wa Afya, Dk. Faustine Ndugulile alipokutana na watafiti wa taasisi hiyo kujadili maambukizi ya ugonjwa wa Corona na aina ya matibabu ambayo wagonjwa wanatakiwa kupatiwa hasa baada ya kubainika kuwa na dalili za ugonjwa huo zinatofautiana na dalili za wagonjwa wa mataifa mengine.
“Kuna mambo mengi tunapaswa kuyafanyia utafiti wa kisanyansi, moja ni uelewa wa jamii, tunataka kujua wagonjwa wanaougua corona ni wagonjwa wa namna gani, wana magonjwa ya aina gani, dalili zinazowapata wagonjwa ni za aina gani. Hapa tunataka tupate uwelewa,” amesema Dk. Ndugulile.
Pia, amesema kupitia utafiti huo wanataka kujua aina za matibabu ambayo wagonjwa wanatakiwa kupatiwa ili kuhakikisha ugonjwa wa Covid-19 unadhibitiwa hapa nchini.
“Kutokana na muitikio mkubwa wa tiba asili na tiba mbadala, kupitia kikao hiki nawaelekeza wataalamu wetu wajipange kufanya utafiti na kutoa majibu ya tiba ya maambukizi ya virusi vya Corona,” amesema Dk. Ndugulile.
Amesema wamekubaliana na watafiti hao kufanyia kazi maagizo hayo ndani ya muda mfupi na kutoa majibu sahihi ambayo yatasaidia katika mapambano ya ugonjwa wa corona.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa NIMR, Prof. Yunus Mgaya amesema mapambano dhidi ya ugonjwa Covid-19 ni vita ambayo inapaswa kufanyiwa utafiti ambao utasaidia kupatikana kwa njia sahihi za kukabiliana na maambukizi ya ugonjwa huo.
“Tunafahamu kwamba jamii za kiafrika zina utaalamu katika miti shamba. Katika hili kuna tafiti mbalimbali zinaendelea ili kuchunguza uwezo wa miti shamba kwa lengo la kupunguza makali ya Covid-19,” amesema.
Leave a comment