RAIS John Magufuli ameagiza Watanzania kuepuka mikusanyiko ikiwa ni hatua za awali kukabiliana na kusambaa kwa virusi vya corona nchini. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Amesema, ugonjwa huo ambao unasambaa kwa kasi duniani kote, ni hatari zaidi ya Ukosefu wa Kinga Mwilini (Ukimwi), huku akisisitiza maeleza yanayotolewa na Wizara ya Afya yazingatiwe.
“Tuepuke mikusanyiko, hata mimi hapa nimefanya makosa kwa sababu nimesimama hapa nimewafanya mkusanyike, ndio maana nataka niondoke harakaharaka ili msiendelee kukusanyika, corona ni mbaya kuliko Ukimwi,” amesema Rais Magufuli leo tarehe 15 Machi 2020, alipokuwa Chalinze, Pwani akielekeza ziarani Morogoro.
Taarifa zaidi kutoka Wizara ya Afya zinaeleza, kwamba mpaka sasa Tanzania haijashuhudia mtu mwenye maambukizi ya virusi hivyo, hata hivyo imeweka mkazi kwa wananchi kuchukua tahadhari ikiwa ni pamoja na kutopeana mikono na kukumbatiana ili kuzuia uwekano wa kusambaa kwa virusi hiyo.
Leo asubuhi Rais Magufuli ametoa agizo la kusitisha mbio za Mwenge na kuagiza fedha zilizotengwa kwa ajili ya kufanikisha zoezi hilo, zipelekwe Wizara ya Afya kwa ajili ya kununua vifaa na dawa za kudhibiti janga la mlipuko wa virusi hivyo.
“Mbio za Mwenge hazitafanyika mpaka tuhakikishe Corona imeisha,” ameagiza Rais Magufuli alipokuwa Ubungo, jijini Dar es Salaam leo asubuhi.
Leave a comment