PROF. Ibrahim Haruna Lipumba, mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), ametoa masharti mazito ya “ushirikiano” kwa viongozi wenzake wa vyama vya ACT- Wazalendo na Chama cha Demokarsia (Chadema), kuelekea uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari, leo Jumatatu, makao makuu ya chama chake, Buguruni, Prof. Lipumba amesema, ili CUF iungane na Chadema na ACT- Wazalendo, ni sharti vyama hivyo, “visipokee mabaki” kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Amesema, “nipo tayari kuungana na Mbowe na Zitto Kabwe, pamoja na vyama vingine vya upinzani, iwapo watakuwa tayari kutekeleza sharti hilo. Vinginevyo, sisi kama CUF tutakwenda kivyetu na wao kivyao.”
Kwa mujibu wa Prof. Lipumba, CUF haiko tayari kuungana na vyama vinavyosubiria wagombea walioenguliwa na kuonekana hawafai katika nafasi mbalimbali ndani ya CCM.
Kiongozi huyo wa CUF ametoa msimamo huo, kufuatia kauli ya Zitto, kwamba vyama vya upinzani havina budi kuungana katika uchaguzi huo, ili viking’oe chama tawala madarakani.
Kupitia mkutano huo, Prof. Lipumba amesema vyama vya upinzania mpaka sasa havijazungumza chochote kuhusu ushirikiano huo.
“Huwezi sema ushirikiano wakati hujaongea na vyama. Unatakiwa ushirikiano wa kuitoa CCM madarakani na sio ushirikiano wa kusubiri mabaki ya CCM.
“Sio utaratibu wa kufanya umoja wa kusubiri nani atakeyetemwa na CCM au kuenguliwa. Tutashirikiana na vyama vyenye nia ya dhati ya kusimamia mabadiliko ya kweli,” ameeleza Prof. Lipumba.
Leave a comment