SELEMANI Jafo, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), amewataka wakuu wa mikoa na wilaya kuchukua hatua dhidi ya watendaji wa serikali wanaowabambikia kesi wananchi, anaandika Dany Tibason.
Jafo alikuwa akijibu swali la Dk. Dalaly Kafumu, Mbunge wa Igunga, Tabora aliyedai kuwa wananchi hususan wa vijijini wamekuwa wakisingiziwa makosa mbalimbali na watendaji wa serikali kutokana na uelewa mdogo wa masuala ya kisheria na haki zao.
Dk. Kafumu aliwatuhumu watendaji wa vijiji na kata ambao alidai wamekuwa wakishirikiana na mahakimu wa mahakama za mwanzo na mabaraza ya ardhi kuwaonea na kuwadhulumu wananchi ikiwemo kuwabambikiza kesi na kuwanyang’anya ardhi.
“Je, ni lini Serikali itachukua hatua za kukomesha tabia hiyo?” alihoji Dk. Kafumu.
Akijibu swali hilo, Jafo alikiri kuwepo na malalamiko dhidi ya baadhi ya watendaji wa kata na vijiji na hivyo kuwaagiza wakuu wa mikoa na wilaya wahakikishe wanasimamia maadili ya watendaji kwa ngazi zilizo chini yao na kuchukua hatua za kinidhamu kwa wanaobambikizia kesi wananchi.
“Watendaji wote katika ngazi zote za mamlaka za Serikali za Mitaa wanatakiwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu katika utekelezaji wa majukumu yao, Serikali haitasita kumchukulia kali mtendaji atakaekiuka sheria, kanuni na taratibu za kazi,” amesema.
Naibu Waziri huyo amesema Serikali itaendelea kuhakikisha inasimamia kikamilifu maadili ya watumishi wa umma kwani ndiyo msingi wa usatawi wa jamii na kwamba hakuna mtumishi wa umma asiye na maadili atakayevumiliwa.
“Nato wito kwa viongozi na wananchi wote nchini kuhakikisha wanawafichua watendaji na watumishi wa umma wenye tabia kama hii ili waweze kuchukuliwa hatua stahiki,” amesema.
Leave a comment