BARAZA la Usalama la Taifa jijini Washington, Marekani limesema linachunguza shambulio kubwa la kimtandao ambalo limekumba mifumo ya kompyuta duniani kote, anaandika Hamis Mguta.
Mamlaka nchini Marekani zimesema zimedhamiria kuwachukulia hatua wahusika wa uhalifu huo wa mtandaoni, uliosababisha makampuni, taasisi mbalimbali pamoja na watu binafsi kupoteza taarifa zao nyeti baada ya shambulizi la kimtandao.
Mashirika mbalimbali zikiwemo taasisi za kifedha, idara za serikali, makampuni makubwa, na kampuni za usafirishaji ni miongoni mwa zilizoathirika ambapo wadukuzi wa mitandaoni walizishikilia na kuzipoteza taarifa mbalimbali za mitandao.
Wamiliki wa mitandao husika waliambiwa na wadukuzi kuwa kompyuta zao zimenaswa mpaka walipe kiasi cha Dola mia tatu za Marekani katika akaunti isiyofahamika. Huku Wizara ya Mambo ya Ndani ya Marekani ikiwashauri watu wasilipe fedha hizo.
Hata hivyo wizara hiyo imesema hakuna uhakika kwamba, mafaili yaliyofungwa yatafunguka baada ya malipo hayo kufanyika.
Shambulio hilo la kimtandao lilianza nchini Ukraine na linaendelea sehemu nyengine duniani na baadhi ya mashirika yanayoripoti tatizo hilo ni pamoja na Benki kuu nchini humo na kampuni ya kuunda ndege ya Antonov na mashirika mawili ya posta.
Kampuni ya mafuta nchini Urusi ya Rosneft na ile ya Denmark ya Maersk ni miongoni mwa zilizokumbwa na shambulizi hilo la kimtandao.
Leave a comment