Tuesday , 7 May 2024
Home Habari Mchanganyiko Nguruwe wapigwa marufuku Morogoro
Habari Mchanganyiko

Nguruwe wapigwa marufuku Morogoro

Nguruwe wakiwa wanazurula mtaani
Spread the love

WAFUGAJI wa nguruwe kwenye kata ya Kingolwila, Morogoro wametakiwa kutoiachia mifugo yao kudhurula hovyo mitaani huku ikitapanya kinyesi hali inayopelekea uchafuzi wa mazingira, anaandika Christina Haule.

Hayo yalibainishwa jana na Diwani wa Kata ya Kingolwira, Bidyanguze Steven katika kikao cha baraza la maendeleo ya kata hiyo ambapo amesema kuwa kumekuwepo na malalamiko mengi toka kwa wananchi kuhusiana na kinyesi cha Nguruwe kuenea kila mahali katika kata hiyo.

Amesema kuwa hali hiyo inatokana na mifugo hiyo kuachwa ikizurula mitaani na kusababisha uchafuzi wa mazingira na kutishia magonjwa ya milipuko.

Bidyanguze amesema kuwa mifugo hiyo imekuwa ikileta usumbufu kwa wananchi hasa kwa ambao imani zao za kidini haziwaruhusu kutumia au kuwepo kwa mifugo hiyo katika nyumba zao hali inayopelekea malalamiko toka kwa wakazi hao.

Hivyo amewataka wafugaji wote wa nguruwe katika kata hiyo kuhakikisha wanawajengea uzio na kuwawekea mazingira mazuri ili kuhakikisha mifugo hiyo haizagai hovyo mitaani na kutapanya kinyesi kila kona.

Hata hivyo amewataka wenyeviti wa mitaa kuhakikisha wanasimamia na kuwaelimisha wananchi wao ili kuweka mazingira katika hali ya usafi.

“Ufugaji uwe wa nyumbani, hakuna kuacha kinyesi wala nguruwe wanazurura hovyo mitaani, wenyeviti tusimamie hili na tuwahimize watu kupunguza idadi ya mifugo ili wabaki na mifugo ambayo wanaweza kuitunza,” amesema Bidyanguze.

Kwa upande wake, Afisa mifugo wa Kata hiyo, James Yuda amesema ni vyema wananchi wakapunguza mifugo na kuepuka kuwa na mifugo mingi wasiyoweza kuimudu na badala yake kuamua kuiacha ijichunge na kutapakaa hovyo mtaani.

Yuda amesema kuwa wananchi wakipatiwa elimu na kufahamishwa faida za kuwa na mifugo michache zoezi ambalo atalisimamia yeye mwenyewe akishikiliana na wenyeviti litapunguza au kuondoa kabisa tatizo la kuzurula hovyo kwa mifugo mitaani.

Wakazi wa kata hiyo wamesema kuwa mifugo hiyo imekuwa tatizo kubwa sana kufuatia kuachiwa ikidhurula mitaani na kwamba harufu ni kali sana inayotoka katika mazizi ya mifugo hiyo.

“Jamani toka lini nguruwe akaachiwa anazurura tu, wanakuja mpaka uani wakikuta vyombo au ndoo ya maji wanaweka midomo yao, kwa kweli ni kero, afadhali watengewe maeneo tofauti na makazi ya watu, wengine mnyama huyu kwetu ni haramu,” amesema Nuru Haniu.

Hata hivyo kufuatia kipindi hiki kuwa ni cha kilimo, mifugo mingine kama bata, kuku, ng’ombe na mbuzi wamepigwa marufuku kuzurura hovyo kutokana na kuharibu mahindi na mazao mengine katika kata hiyo.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

AfyaHabari MchanganyikoMakala & Uchambuzi

Kisukari cha mimba ni nini?

Spread the loveKisukari cha mimba ni aina ya kisukari kinachotokea kwa baadhi...

Habari Mchanganyiko

Mafunzo kwa bodaboda 395 yamkuna Meya Dodoma

Spread the loveNAIBU Meya wa Jiji la Dodoma, Asma Karama amepongeza mafunzo...

Habari Mchanganyiko

Samia aagiza huduma za dharura maeneo yaliyoathiriwa na kimbunga Hidaya

Spread the love   RAIS wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, Samia...

Habari Mchanganyiko

Mahakama yatoa uamuzi zuio dhidi ya Club House

Spread the loveMAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu jijini Dar es Salaam,...

error: Content is protected !!