WATU wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wameiteketeza kwa moto nyumba ya Bakari Msanga, mwenyekiti wa kijiji cha Jaribu Mpakani wilayani Rufiji, Mkoa wa Pwani, kwa nia ya kutaka kumdhuru, anaandika Faki Sosi.
Wanakijiji wamesema watuhumiwa wa tukio hilo waliifikia nyumba hiyo kiasi cha saa 1 usiku na kukuta wapangaji ambao ni walimu wawili na wanafunzi watatu wa Chuo cha Uuguzi Kairuki waliokwenda kufanya mazoezi ya vitendo kwenye zahanati ya Jaribu Mpakani.
Misana Sabatho, mwalimu wa Sekondari ya Mjawa karibu na eneo hilo, ni mmoja wa wapangaji waliokuwepo wakati wavamizi walipofika nyumbani kwa mwenyekiti huyo.
Sabatho amesimulia mkasa huo kwa MwanahalisiOnline akisema alikuwa na mdogo wake pamoja na mwalimu mwenzake waliopanga nyumba hiyo, wakati wavamizi walipofika na kuingia ndani haraka baada ya kukuta mlango uwazi.
ndani kutokana mlango ulikuwa wazi ambapo alitakiwa kusalimu amri zao mara baada ya kumweka chini ya ulinzi na watu hao walivamia kwenye nyumba hiyo na siraha.
“Walituweka chini ya ulinzi mimi na mdogo wangu na mwalimu mwenzangu aliyepanga kwenye nyumba hii na kuuliza wapi alipo Bakari Msanga mwenyekiti wa Kijiji… walikuwa na silaha,” alisema.
“Sisi tulijibu hatujui aliko mwenyekiti. Waliendelea na kuvunja milango ya vyumba katika nyumba tunayoishi na kuanza kumwaga mafuta ya petroli kwenye kuta na sehemu zote za nyumba,” ameeleza mwalimu Sabatho.
Wakati harakati za wavamizi hao zikiendelea, wapangaji wengine waliokuwa kwenye shughuli zao za mafunzo kwa vitendo, waliwasili nyumbani hapo na kuishia kudhibitiwa kwa kuwekwa chini ya ulinzi wa wavamizi.
Mpangaji mmoja alikimbia, alisema mwalimu Sabatho ambaye pia alisema wavamizi ambao aligundua baadaye kuwa walifika hapo kwa pikipiki aina ya Boxer, waliondoka kabla ya kusimamia kuona kama moto ulishashika nyumba yote.
Ramadhani Ngaruma, Mtendaji wa Kata ya Mjawa, amethibitisha kuwa tukio hilo limetokea kwenye eneo lake la uongozi, na “nimesikitishwa sana na kitendo hiki cha kinyama na ishara ya kutokuwepo kwa amani hasa kwa kuwa wamekuja kwa ajili ya mwenyekiti wa kijiji.”
Akinukuu mashuhuda, Ngaruma amesema wavamizi walikuwa wamejifunika usoni, staili aliyosema kuwa ilitumika mwaka jana katika tukio la watu wasiojulikana kufika na kumsaka mtendaji wa kijiji hicho aliyemtaja kuwa ni Maulidi Msafa.
Alisema Msafa alikimbia makazi yake baada ya kupata taarifa za kutafutwa na watu wa aina hiyo.
Ali Jabiri, Mwenyekiti wa Kitongoji cha Jaribu Mpakani, ameeleza kuwa viongozi na wananchi wanahofu kutokana na matukio hayo ya kuwindwa kwani tayari viongozi wawili wa eneo hilo wameyakimbia makazi yao.
Viongozi wa ngazi ya juu wa polisi pamoja na serikali ya wilaya ya Rufiji waliwasili eneo la tukio kufuatilia kilichotokea. Hakuna taarifa zaidi zilizopatikana kuhusiana na kauli ya serikali.
Leave a comment