SHIRIKA la Afya Duniani (WHO) linatarajiwa kuipatia Serikali ya Tanzania fedha Sh 855 milioni kwa ajili ya kuwezesha kufanya utafiti wa kitaifa wa viashiria vya magonjwa yasiyoambukiza (Steps Survey 2023) unaotarajiwa kuanza mapema Agosti, mwaka huu nchi nzima. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanywa na Waziri wa Afya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Nassor Mazrui jijini Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), Prof. Said Abood amesema fedha hizo zitazaidia kukamilisha zoezi hilo kwa Tanzania Bara na Zanzibar.
Prof. Abood amesema kuwa Utafiti wa “Steps Survey” ni ufuatiliaji wa viashiria vya magonjwa yasiyoambukiza ili kukusanya takwimu muhimu kuhusu magonjwa yasiyoambukiza na viashiria vya hatari vya magonjwa hayo.
“Tafiti hii itatoa taarifa muhimu kuhusu hali ya afya na jamii yetu na kutambua matendo ya maboresho katika afya na kuweka mikakati kwa ajili ya kuboresha Matendo hayo kwa lengo la kuimarisha afya ya Jamii yetu,” amesema Prof. Abood
Amesema takwimu ndio kiini cha kujenga Taifa lenye afya bora. “Takwimu tutakazokusanya kupitia Utafiti huu zitatumika kama dira ya kutuongoza kuelekea kutengeneza mikakati yenye ushahidi ili kuboresha afya za watanzania.
Vile vile alisema takwimu zitawafanya kuelewa viashiria vya hatari vya magonjwa yasiyoambukiza kama vile ulaji usiofaa, kutokufanya mazoezi ya mwili na unywaji wa pombe kupita kiasi na kunaweza kubuni mbinu zitakazoshughulikia visababishi hivyo vikuu vya NCDs.
Naye, Mwakilishi wa WHO Dk. Alphoncina Nanai amesema magonjwa yasiyoambukiza yameanza kuwa tatizo kubwa ulimwenguni.
Amesema katika kila vifo 10, vifo saba vinasababishwa na magonjwa yasiyoambukiza ulimwenguni na watu milioni 17 wanafariki ambapo asilimia 86 ya vifo vinatoka nchi za Afrika.
Aidha, Dk. Nanai amesema magonjwa yasiyoambukiza yanaweza kuzuilika ndipo WHO na Serikali ilianzisha utaratibu wa kupima miaka 10 iliyopita ili kujua uzito wa magonjwa hayo na yanakuaje.
Amesema wanafuatilia magonjwa hayo kwani wapo watu wengi hawajui kama wana magonjwa hayo, magonjwa hayo kwa Sasa yanaua watu wengi
Amesema WHO itaendelea kushirikiana na Serikali ili kujua namma gani wataweza kuzuia magonjwa hayo kwa yeyote ambaye hajapata basi asipate na aliyepata aweze kutumia vizuri dawa
Akizungumzia utafiti huo, Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge Huduma Za afya na Masuala ya UKIMWI, Stanislaus Nyongo amesema utafiti huo utaenda kutatua changamoto la tatizo la magonjwa hayo na kuipa nchi dira.
Amesema kama Bunge wapo tayari kuelimisha wananchi kuepukana na magonjwa hayo ambayo hivi Sasa yanatumia pesa nyingi kuyatibu.
Mining Census 2023
Watanzania mnakaribishwa kwenye SENSA ya Madini 2023 yenye lengo la kujua idadi ya migodi Tanzania, Idadi ya wachimbaji au watanzania wanaoshughulika na sekta ya Madini, Hali ya uchimbaji wa madini (zana zitumikazo kwa kila mgodi, aina ya teknolojia) na mapendekezo ya mbinu za kuboresha Sekta ya Madini.