CHUO Kikuu cha Kumbukumbu ya Hubert Kairuki (HKMU), kimeiomba serikali itoe ruzuku kwa vyuo vikuu vinafsi ili kuvijengea uwezo kuboresha miundombinu yake, kusomesha wahadhiri na mifumo yake ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA). Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Ombi hilo lilitolewa mwishoni mwa wiki na Makamu Mkuu wa chuo hicho, Profesa Yohana Mashalla, wakati akizungmza kwenye mahafali ya 21 ya chuo hicho yaliyfanyika Mikocheni .
Kwenye mahafali hayo, wahitimu walikuwa 308 waliopata Shahada katika fani za udaktari, ustawi wa jamii, uuguzi, Shahada za Uzamili na shahada ya Heshima ya Sayansi.
Alisema kupitia mpango wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Uchumi ambapo vyuo vikuu vya serikali vimewezeshwa kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujenga kampasi mpya maeneo mbalimbali nchini.
Profesa Mashalla alisema upanuzi huo haukujumuisha vyuo vikuu vya binafsi na vingi vitaendelea kuwa na ubaha wa nafasi za kufundishia hivyo kushindwa kupunguza changamoto ya wahitimu wa elimu ya sekondari.
Profesa Mashalla alisema pamoja na changamoto mbalimbali lakini chuo kimeendelea kusomesha wahadhiri wake katika ngazi za Uzamili na Uzamivu ndani na nje ya nchi.
Alisema kwa sasa wana wahadhiri 16 walioko masomoni na kati ya hao, tisa wanasomea Shahada za Uzamivu na saba Shahada za Uzamili na kamba wahadhiri tisa wanasoma nchini na saba wako vyuo vya nje ya nchi.
Aliishukuru Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kufadhili wanataaluma wanne wa chuo hicho kupitia program ya Higher Education for Economic Transformation kwa masomo ya Uzamili na Uzamivu.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Mtandao wa Elimu ya Afya Kairuki (KHEN), Kokushubira Kairuki, alisema sababu kubwa ya kuwekeza kwenye sekta ya afya ni ubaha mkubwa wa rasilimali watu katika sekta hiyo.
“Kutokana na maono ya KHEN ambayo ni kuboresha hali ya maisha ya binadamu sisi waanzilishi wa KHEN tuliona njia bora ya kukabili changamoto hiyo ni kuwekeza vilivyo kwenye mafunzo ya rasilimali watu kwenye sekta ya afya,” alisema
Alisema tangu chuo kianzishwe mwaka 1997, chuo kimechangia wataalamu katika sekta ya afya na ustawi wa jamii wapatao 5,413 na wengi wa wahitimu hao wako kwenye taasisi mbalimbali binafsi na za umma wakitoa huduma za afya.
”Wito wangu kwa Serikali yetu tukufu ni kuendelea kuweka mazingira rafiki yatakayochagiza uanzishwaji wa vyuo vikuu vingi zaidi vinavyotoa mafunzo ya wataalamu wa sekya ya afya kukabiliana na changamoto ya maradhi kwasababu mahitaji bado ni makubwa kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Afya Duniani,” alisema
Aliishukuru taasisi ya Health Reach ya Canada kwa kuendelea kutoa misaada ya kifedha kwa baadhi ya wanafunzi wahitaji kwa miaka kadhaa sasa na familia ya raia wa Marekani Benjamin Christensen ambayo nayo imekuwa ikitoa misaada kama hiyo.
Leave a comment