UTAWALA wa Rais wa Marekani, Donald Trump umetishia kuchukua hatua kali dhidi ya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Kivita (ICC), ikiwemo kuwawekea vikwazo majaji wake endapo wataendelea na uchunguzi juu ya madai ya uhalifu wa kivita uliofanywa na Wamarekani nchini Afghanistan. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Vile vile, imetishia kufunga Ofisi ya Shirika la Uhuru wa Palestina (PLO) iliyoko mjini Washington bila ya wasiwasi, kufuatia uwepo wa madai ya Palestina kujaribu kushinikiza uchunguzi wa mahakama ya ICC dhidi ya taifa la Israel ambalo ni mshirika mkubwa wa Marekani.
Mshauri wa Rais Trump kuhusu masuala ya usalama wa taifa hilo, John Bolton anatarajiwa kutoa msimamo wa Marekani mchana wa leo, ambapo kwa mujibu wa mtandao wa Reuter, umeripoti kuwa sehemu ya hotuba inayotarajiwa kutolewa na Bolton, inaeleza kwamba, Marekani iko tayari kutumia njia yoyote kulinda raia na washirika wake wanaotuhumiwa na mahakama ya ICC.
“Marekani itatumia njia yoyote itakayolazimika kutumia ili kulinda raia wetu na washirika wetu kutokana na mashtaka yasiyo ya haki na mahakama isiyo rasmi,” inaeleza sehemu ya hotuba hiyo.
Hotuba hiyo inaeleza kuwa, Marekani italipa kisasi endapo mahakama ya ICC itatekeleza azimio lake la kufungua uchunguzi huo juu ya madai ya uhalifu wa kivita uliofanywa na washirika wa Marekani pamoja na maafisa intelijensia wake katika vita iliyotokea nchini Afghanistan.
Inaelezwa kuwa, iwapo mahakama ya ICC itaendelea na msimamo wake,Marekani itazuia majaji na waendesha mashtaka wake kuingia nchini humo, pamoja na kusitisha kutoa msaada ikiwemo wa kifedha katika mahakama hiyo.
Leave a comment