UCHAGUZI Mkuu katika Taifa la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) upo njia panda baada ya mamlaka za nchi hiyo kujiumauma. Vinaripoti vyombo vya kimataifa … (endelea).
Uchaguzi huo ulipangwa kufanyika Jumapili wiki hii ambapo sasa kauli zinazotolewa na mamlaka za DRC zinajielekeza katika kuahirisha uchaguzi huo licha ya kauli ya awali kudai kuwa, uchaguzi ungefanywa ndani ya muda uliopangwa.
Ceni Jean-Pierre Kalamba ambaye ni msemaji wa tume ya uchaguzi nchini humo ameeleza kuwa, hakuna uwezekano wa uchaguzi huo kufanyika Jumapili ya wiki hii kama ulivyopangwa.
Kauli yake ni tofauti na ile ya kwanza iliyotolewa wiki iliyopita baada ya ghala la kuhifadhia vifaa vya uchaguzi liliopo jijini Kinshasa kuungua na kuteketeza vifaa hivyo kwamba, uchaguzi usingeahirishwa.
Kauli iliyotolewa jana Jumatano inaeleza kuwa, maandalizi bado ni hafifu na hayajakamilika kutokana na tukio la uunguaji ghala hilo. Hata hivyo leo ilitarajiwa serikali kutoa msimamo wake kuhusu uchaguzi huo.
Ni zaidi ya miaka miwili sasa uchaguzi wa DRC umekuwa ukisogezwa mbele kutokana na Rais Joseph Kabila kung’ang’ania madaraka kwa kutoa visingizio mbalimbali.
Unyanyapaa wa viongozi wa upinzani DRC unaendelea kufanyika ambapo polisi nchini humo wamemzuia mmoja wa wagombea wakuu wa upinzani wa kiti cha urais, Martin Fayulu kuzindua kampeni zake katika mji mkuu wa nchi hiyo.
Tayari kuna tangazo la kupiga marufuku ya mikutano ya kisiasa ambapo Gavana wa Mji wa Kinshasa, Andre Kimpita, alisema kuwa hatua hiyo ya kupiga marufuku mikutano ya siasa imechukuliwa kwa sababu za kiusalama. Hatua hiyo imekasirisha zaidi wapinzani.
Leave a comment