RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli amewahimiza wananchi kulipa kodi ili kuiwezesha serikali kulipa mikopo inayokopa kwa ajili ya kufanikisha ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Rais Magufuli ametoa wito huo leo tarehe 20 Desemba 2018 jijini Dar es Salaam, katika sherehe za uwekaji jiwe la msingi katika ujenzi wa daraja la kisasa la Selander litakalopita juu ya bahari.
“Kodi ni muhimu sana, ambazo tunastahili kulipa tulipe, hii mikopo tunayokopa italipwa kwa kodi,” amehimiza Rais Magufuli.
Naye Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwele amesema ifikapo mwishoni mwa mwezi Januari mwakani, tiketi za mabasi zitatolewa kwa njia ya kielektroniki ili kurahisisha ukusanyaji wa kodi na kuongeza mapato ya serikali.
“Katika usafirishaji upande wa barabara, nchi yetu ukiacha maroli, ina mabasi 49,000 mabasi, katika mabasi hayo, 7,000 yanasafiri kwenda mikoani yanayobaki ni daladala, Dar es Salaam ina daladala 9,000, tayari wizara yangu inaendelea na mazungumzo ili kujua tunapataje mapato,” amesema na kuongeza Mhandisi Kamwele.
“ Hapa ukataji tiketi bado uko kienyeji, nimeongea na katibu mkuu wa hazina kwamba ikifika Januari mwishoni mabasi yote tiketi iwe ya kielektroni, tutakusanya kodi kwa urahisi bila ubabe.”
Akizungumza kuhusu daraja hilo, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mhandisi Patick Mfugale amesema daraja hilo litakuwa na njia nne za magari na sehemu ya waenda kwa miguu ambalo litadumu zaidi ya miaka 100.
“Daraja hili lina uwezo wa kubeba tani 180 kwa wakati mmoja, daraja hili pamoja na barabara unganishi litakuwa na urefu wa kilometa 6.23,” amesema Mhandisi Mfugale
Leave a comment