MWENYEKITI wa Chadema, Freeman Mbowe na mbunge wa chama hicho katika jimbo la Tarime Mjini, Esther Matiko, waweza kulazimika kulia sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya ndani ya gereza kuu la Segerea. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Wanasiasa hao wawili na wengine saba, wamefikishwa mahakamani na serikali, Februari mwaka huu. Wanatuhumiwa kwa makossa ya uchochezi, uvunjifu wa amani, maandamano na kusababishia mauaji, aliyekuwa mwanafunzi wa chuo cha usafirishaji cha taifa (NIT), Akwiline Akwilina.
Mwanafunzi huyo wa mwaka wa pili, aliuawa kwa kupigwa risasi na polisi, Februari mwaka huu, katika maeneo ya Mkwajuni jijini Dar es Salaam.
Wakati washitakiwa wengine wakiwa nje kwa dhamana, Mbowe na Matiko, wako gerezani, kufuatia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kuwafutia dhamana zao, Novemba mwaka huu.
Washitakiwa wengine kwenye kesi hiyo, ni Dk. Vicenti Mashinji, katibu mkuu wa chama hicho; John Mnyika, mbunge wa Kibamba na naibu katibu mkuu wa chama hicho Bara na Salum Mwalimu, naibu katibu mkuu Zanzibar.
Wengine, ni Halima James Mdee, mwenyekiti wa Baraza la Wanawake (BAWACHA) na mbunge wa Kawe; Ester Bulaya, mbunge wa Bunda; Mchungaji Peter Msigwa, mwenyekiti wa Kaanda ya Nyanda za Juu Kusini na mbunge wa Iringa Mjini na John Heche, mbunge wa Tarime Vijijini.
Hakim Mkuu Mkazi wa Mahakama Kisutu, Wilbrod Mashauri ameeleza mbele ya mawakili wa serikali na wale wa utetezi, kwamba kwa kuwa shauri hilo limeletewa mbele yake kwa ajili ya kutajwa, basi anaipanga kesi hiyo, 3 Novemba mwakani.
Alisema, mahakama yake imefungwa mikono kuendelea kusikiza shauri hilo kwa kuwa watuhumiwa walikata rufaaa Mahakama Kuu na kwamba mahakama yake haijapokea maelekezo yeyote kutoka Mahakama Kuu wala Mahakama ya Rufaa.
Mbowe na Matiko walitangazwa kwenye mkutano wa “kutafakari hali ya kisiasa nchini,” uliofanyika Unguja, wiki iliyopita na kuhudhuriwa na viongozi wa vyama sita vya upinzani, kuwa “wafungwa wa kisiasa.”
Mkutano wa tafakuri ya kisiasa nchini, uliitishwa na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad. Ulihudhuriwa na viongozi kadahaa, wakiwamo mawaziri wakuu wawili wastaafu, Edward Lowassa na Fredrick Sumaye.
Mwingine aliyehudhuria mkutano huo, ni Kiongozi Mkuu wa chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Zuberi Kabwe.
Leave a comment