NAIBU Spika wa Bunge, Azzan Zungu, amesema kilichofanya Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, achaguliwe kuwa Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) ni uadilifu, kujiamini na nidhamu yake, pamoja na hatua ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kuimarisha diplomasia na mataifa ya nje. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Zungu ametoa kauli hiyo leo tarehe 30 Oktoba 2023, katika hafla ya kumpokea Spika Tulia, aliyewasili nchini akitokea Angola, ambapo uchaguzi ulifanyika Ijumaa iliyopita.
“Sifa za mtu kushinda hashindi sababu ya kujua, katika waliokuwa wanamsaidia Spika wanauliza kwa nini yeye tukawaambia vitu vitatu. Uadilifu, kujiamini na nidhamu. Majibu aliyokuwa anayajibu yamewafanya watu waingiwe na aibu. Wenzake walikuwa kama ni wanaharakati wakisema mtu na mikono mimi niko hivi akiulizwa swali la maana hana jibu,” amesema Zungu.
“Lakini kubwa ni Mungu na msaada kutoka kwa Rais wetu Dk. Samia, lakini yeye akajiongeza. Majibu ya mazingira anayo, haki za binadamu yapo, demokrasia duniani iko kichwani atakosa ushindi huyo?”
Dk. Tulia alishinda baada ya kupata kura 172 kati ya 303, zilizopigwa na wajumbe wa IPU, wakati washindani wake, Catherine Hara kutoka Malawi akipata kura 61. Mergane Kanoute wa Senegal akipata kura 59, huku Abdibadhir Hagi wa Somalia, akiambulia kura 11.
Leave a comment