KIONGOZI Mkuu wa Chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe amesema Katibu Mkuu wa chama hicho, Ado Shaibu atavaa viatu vyake vya uongozi pindi itakapotokea akafariki. Anaripoti Mwandishi Wetu, Tunduru … (endelea).
Amesema malengo ya chama hicho ni kushika dola hivyo kwa hatua waliyofikia na namna alivyomuandaa Ado ana uhakika kuwa atakiongoza chama hicho kuchukua madaraka.
Zitto ametoa kauli hiyo jana tarehe 13 Machi 2023 wakati akihutubia wananchi wa Tunduru mkoani Ruvuma katika mkutano wa hadhara.
Amesema; “Mimi ni kiongozi wa chama hiki, nina matamanio ya kuona nakipeleka chama kushika dola, lakini Mwenyezi Mungu naye ana mipango yake.
“Hata ikitokea leo Mwenyezi Mungu amesema bwana siku zako zimefika sasa nakuita, nitakwenda kwenye nyumba yangu ya milele nikiwa natabasamu,” amesema.
Amesema atakwenda akiwa anaamini kwamba ameacha mtu atakayeendeleza mapambano kama ambavyo Oliver Tambo alivyomuachia Nelson Mandela –(Afrika Kusini) au kama ambavyo Eduardo Mondlane alivyomuachia Samora Machel (Msumbiji) na huyo mtu ni Ado Shaibu.
Amewaomba wananchi hao kuwa ACT Wazalendo kiwe chama chao na sio suala la mjadala kufanya uamuzi tena.
Amesema chama hicho ndio chama kilichowathamini wana Tunduru kwa kumshika mkono mtoto wao (Ado) na kumpa majukumu mazito.
“Sasa nasema hata Mwenyezi Mumgu akinichukua sina wasiwasi… Ado atavaa viatu vyangu, ataendeleza mapambano mpaka tutakaposhika madaraka,” amesema.
Leave a comment