WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa ameipongeza Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa kuandaa mbio za NBC Marathon ambazo zinalenga kukusanya fedha kwa ajili ya kusaidia afya ya uzazi na saratani ya shingo ya kizazi. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Akizungumza muda mfupi baada ya mbio hizo kumalizika jijijini Dodoma leo Jumapili, Waziri Mkuu amesema Serikali inatambua na kuthamini mchango wa sekta binafsi katika kuiunga mkono kwenye kutatua changamoto mbali mbali zinazoikabili jamii.
“Serikali inathamini mchango mkubwa unaotolewa na benki ya NBC. Tunafurahishwa na ushirikiano mzuri kati ya Taasisi ya Kansa ya Ocean Road, Taasisi ya Benjamini Mkapa pamoja na chama cha riadha Tanzania ambao umekuwa ukiwezesha kukusanya fedha kwa ajili ya kusaida mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi na mwaka huu likiongezeka eneo la afya ya uzazi. Serikali inapongeza jitihada hizi nzuri,” amesema.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya NBC, Theobald Sabi amesema baada ya kumalizika kwa mbio z mwaka huu, benki hiyo inayo furaha kuandaa mbio za mwaka ujao ikiwa ni baada ya kuandaa mbio hizo kwa mara tatu mfululizo kwa ufanisi.
“Baada ya kuandaa mbio hizi kwa mara ya nne mfululizo, tunayo furaha kuanza maandalizi ya msimu wa nne. Fedha zilizopatikana leo shilingi milioni 500 zitatumika kusaidia mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi,” amesema.
Ameongeza “Tunaendelea na jitiahada za kuunga mkono mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi. Mpaka sasa tumefanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi milioni 500 zilizosaidia kufikia upimaji wa saratani ya shingo ya kizazi kwa wanawake zaidi ya 23,500 na matibabu kwa zaidi ya wanawake 1,300.
“Benki ya NBC inawapongeza na kuwashuru washiriki wote kutoka nje na ndani ya nchi kwa kuweza kufanikisha mbio za mwaka huu,” amesema.
Leave a comment