WAZABUNI waliofanyakazi na Halmashauri ya Liwale na kushindwa kulipwa fedha zao, wamembebesha mzigo Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Paul Makonda ili walipwe madai yao. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Makonda ambaye anatarajia kuendelea na ziara yake mkoani Lindi, anasubiriwa kwa shauko kubwa na wazabuni hao ili watoe kilio dhidi ya viongozi wa wilayani Liwale wanavyowatesa na kuwanyanyasa kwa kuwapa kazi bila malipo.
Wazabuni ni Maarifa Nampela, Ally Mchekenge na Hamis Nampela ambao kwa nyakati tofauti wamefanyakazi na Halmashauri ya wilaya ya Liwale, lakini hawajalipwa fedha zao kwa kile kinachoelezwa chuki za baadhi ya viongozi.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Maarifa Nampela anadai sh. milioni 22.6 kati ya sh. milioni 47,7 alizotoa vifaa vya ujenzi kwa ajili ya ukarabati wa Hospitali ya Halmashauri ya Newala.
Halmashauri hiyo imegoma kulipa kiasi cha fedha kilichosalia kwa madai kuwa mzabuni huyo aliingia mkataba na baadhi ya watumishi na sio serikali.
Hata hivyo ripoti ya Mkaguzi wa ndani kuhusu sakata hilo, ameshauri mzabuni huyo alipwe fedha zake.
Licha ya mkaguzi kubaini uwepo deni hilo, Mkuu wa wilaya ya Liwale Goodluck Mlinga amemtaka mzabuni huyo aende mahakamani kwani ameshindwa kumsaidia.
Mzabuni mwingine ni Hamis Ally Nampela mbaye mwaka 2020, Halmashauri ya Liwale iliingia mkataba wa kutumia gari lake kwa ajili ya kusambaza vifaa vya uchaguzi mkuu.
Hata hivyo gari hilo lenye namba za usajili T. 610 BJN Toyota Noah lilikodiwa kwa ajili ya usafirishaji wa vifaa vya uchaguzi, lilichomwa moto kwenye vurugu katika kijiji cha Kibutuka.
Wakati mfanyabiashara huyo akiikaba koo halmashauri imlipe fidia kwa uhalibifu wa gari lake, Katibu Tawala wilaya hiyo, Alexander Marera amegoma kulipa fidia hiyo kwa madai kuwa anapaswa kulipwa na Bima.
Akizungumza na Gazeti hili, Nampela, alisema amehangaka kupata malipo ya fidia ya gari lake bila mafanikio na amekuwa akipewa majibu ya kukatisha tamaa.
“Gari langu limekodishwa kwa mkataba halali, lakini limechomwa moto likiwa mikononi mwao. Bima gani itakubali kulipa fidia kwa gari lililochomwa moto kwenye vurugu. Namsubiri Makonda aje amalize utata huu,” alisema.
Mzabuni mwingine ni Said Mchekenge ambaye aliingia mkataba na Halmashauri hiyo wa kujenga vibanda 11 vya biashara, lakini tangu alipokamilisha ujenzi huo hajalipwa fedha zake.
Alisema vibanda vimechukuliwa na halmashauri na vimepangishwa kwa wajasiriamali na fedha zote zinakusanywa na Halmashauri hiyo kinyume na makubaliano.
Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Zainabu Telack akizungumzia madai ya wazabuni hao alisema anajua mzabuni mmoja ndiye mwenye matatizo, lakini wawili hana taarifa zao.
Hata hivyo aliwataka mkuu wa wilaya na mkurugenzi wake kushughulikia na kumaliza madai yao.
Leave a comment