KADA wa Chama cha ACT-Wazalendo, Ndolezi Petro amerejesha fomu ya kuomba kugombea uenyekiti wa ngome ya vijana ya chama hicho, na kutaja vipaumbele vyake nane alivyoahidi kutekeleza endapo atashinda kinyang’anyiro hicho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Ndolezi amerejesha fomu hiyo leo tarehe 20 Februari 2024, katika makao makuu ya ACT-Wazalendo, akiwa na mgombea wake mwenza katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa ngome hiyo, Malik Juma.
Vipaumbele alivyotaja Ndolezi ni pamoja na kuiunganisha ngome hiyo kuwa moja na yenye kushirikiana kuanzia ngazi za chini mpaka juu. Kuendeleza mazuri yaliyofanywa watangulizi wake na kuboresha mapungufu ili kuongeza ufanisi wake.
Vingine ni, kuifanya ngome kuwa jukwaa na kimbilio la vijana wa Tanzania kupaza sauti zao juu ya changamoto zinazowakabili.Kupigania baraza la vijana Tanzania, kushawishi vijana wengi kujiunga na ACT-Wazalendo na kutoa elimu kwa vijana wa kitanzania juu ya ahadi za chama chake kwa bara na visiwani.
“Vipaumbele vyangu vingine ni kuimarisha mtandao wa chama mikoa yote na kuendelea kufanya kazi ya kuhamasisha usajili wa Wanachama Katika mfumo wa Kidigitali (ACTKiganjani).Kuifungua Ngome kimahusiano ya kidiplomasia na vyama mbalimbali ndani ya Nchi na Nje ya Nchi sambamba na Taasisi mbali mbalimbali,” amesema Ndolezi.
Uchaguzi wa Ngome ya Vijana ya ACT-Wazalendo, unatarajiwa kufanyika tarehe 29 Februari 2024, ambapo mbali ya Ndolezi , wengine waliojitosa kugombea nafasi hiyo ni Abdul Nondo anayetetea kiti chake na Julius Massabo.
Leave a comment