MAELFU ya wafuasi na wanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), wamejitokeza katika maandamano ya amani ya kudai katiba mpya na tume huru ya uchaguzi, yaliyoandaliwa na chama hicho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya…(endelea).
Maandamano hayo ya awamu ya tatu, yaliyotanguliwa na yaliyofanyika jijini Dar es Salaam na Mbeya, yamefanyika leo tarehe 20 Februari 2024, katika njia mbili, msafara wa kwanza uliyoanzia Mbalizi jijini humo, umeongozwa na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe.
Wakati msafara wa pili ulioanzia Uyole jijini humo, uliongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Chadema Bara, Tundu Lissu.
Mbali na kutumia maandamano hayo kudai katiba mpya na tume huru ya uchaguzi, Chadema inayatumia kutoa wito kwa Serikali, kutatua changamoto za ugumu wa maisha unaosababishwa na mfumuko wa bei.
Katika maandamano hayo, baadhi ya washiriki waliimba nyimbo zilizokusudia kufikisha kilio cha ugumu wa maisha kwa Serikali. Sehemu ya nyimbo hizo zilisema; “ili mafuta yasipande bei, sukari isipande bei, watanzania tuamue kwa pamoja tusirudi nyuma.”
Wengi wao walikuwa wamevalia sare za Chadema huku wakiwa wamebeba bendera za chama hicho.
Wakati wakitangaza maandamano hayo, viongozi wa Chadema walisema yatakuwa hayana kikomo hadi pale Serikali itakapofanyia kazi mapendekezo yao.
Leave a comment