MWENYEKITI wa Bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA), Stephen Wassira, amesema kitendo cha baadhi ya taasisi za Serikali kusaini mikataba mibovu bila kujali maslahi ya umma, kinapoteza uaminifu wa wananchi kwa viongozi wanaowaongoza. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Wassira ametoa kauli hiyo leo tarehe 20 Aprili 2023, jijini Dar es Salaam wakati akichangia mada katika mkutano wa Msajili wa Hazina na viongozi wa taasisi, mashirika na wenyeviti wa bodi za mashirika ya umma, uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Akitoa mfano kuhusu ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kwa 2021/22, amesema inatia aibu kuona mkataba wa mradi mkubwa kama wa ujenzi wa reli ya kisasa SGR unaitia hasara serikali.
“Sijui matatizo yetu yanatokana na nini? Kila siku kuna mikataba mibovu na hii inaharibu uaminifu wa wananchi wa Serikali,” amesema Wassira.
Mwanasiasa huyo mkongwe nchini, amehoji kama kitendo cha baadhi ya taasisi kama Shirika la reli Tanzania (TRC) kutoa zabuni kwa wakandarasi wenye gharama kubwa na kuacha wenye gharama ndogo, ni ukosefu wa elimu ya majadiliano au wizi.
“Tumesikia CAG anasema katika ujenzi wa reli wametoa tenda ambayo ingekuwa na thamani ya Sh. 600 bilioni, alikuwa mkandarasi mmoja wameingia akasema atatoa Sh. 1.7 trilioni halafu huyo akachukuliwa. Sasa huu ni ukosefu wa elimu ya kujadiliana au ni wizi? Unasema uende kwenye public utawaambia watanzania ulifanyaje mpaka ukatoka Sh. 600 bilioni mpaka Sh. 1.7 trilioni,” amesema Wassira.
Katika hatua nyingine, Wassira ameshauri tume ya mipango ya taifa iundwe ili kuwezesha viongozi wapya kuendeleza mambo yaliyoanza kufanywa na watangulizi wao.
“Kuwe na tume ya mipango ambayo itakuwa na kazi ya kupanga na uwekezaji, ambayo jambo jema kwa mawazo tungekuwe na vitu endelevu sio kila mtu anayekuja anachukua cha kwake, mwingine akija anafuta. Tunapata shida kidogo, amesema Wassira.
Leave a comment