TOFAUTI na miaka iliyopita, katika matokeo ya Mtihani wa Kumaliza Elimu ya Msingi 2023 (darasa la saba) yaliyotangazwa leo na Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), yameonesha ufaulu wa wavulana na wasichana umefanana ambapo wavulana wamefaulu kwa asilimia 80.59 na wasichana wamefaulu kwa asilimia 80.58. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Matokeo hayo yaliyotangazwa leo Alhamisi na Katibu Mtendaji wa NECTA, Dk. Said Mohamed, jumla ya watahiniwa 1,092,960 sawa na asilimia 80.58 ya watahiniwa 1,356,296 wenye matokeo ya Mtihani wa Kumaliza Elimu ya Msingi 2023 wamefaulu ambapo wamepata madaraja ya A, B, na C.
Wavulana waliofaulu ni 507,920 sawa na asilimia 80.59 na wasichana waliofaulu ni 585,040 sawa na asilimia 80.58.
Mwaka 2022 watahiniwa waliofaulu walikuwa ni 1,073,402 sawa na asilimia 79.62. Hivyo, ufaulu wa jumla umeongezeka kwa asilimia 0.96.
Katika ubora wa ufaulu, watahiniwa wengi wamepata daraja la B na C ambapo daraja la B ni watahiniwa 314,646 (23.20%), daraja la C ni watahiniwa 724,371 (53.41%). Aidha, watahiniwa 53,943 (3.98%) wamepata daraja la A.
Ubora wa ufaulu kwa wasichana umeongezeka kwa kiasi kikubwa hadi asilimia 80.58 ikilinganishwa na asilimia 78.91 katika mwaka 2022 ambapo ongezeko katika daraja la A ni asilimia 0.13, daraja la B ni asilimia 0.96 na daraja la C ni asilimia 0.57.
Ubora wa ufaulu kwa wavulana umeongezeka hadi asilimia 80.59 ikilinganishwa na asilimia 80.41 katika mwaka 2022 ambapo ongezeko katika daraja la A ni asilimia 0.42 na daraja la B ni asilimia 0.58. Aidha, ufaulu wa daraja la C umeshuka kwa asilimia 0.83.
Leave a comment