BAADHI ya wananchi wa Kata ya Kivule, wamembana mbunge wao (Ukonga), Jerry Silaa, kuhusu utatuzi wa changamoto sugu zinazowakabili ikiwemo ubovu wa barabara na askari wa akiba (mgambo) kusumbua wafanyabiashara ndogondogo (wamachinga). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Tukio hilo lilitokea jana tarehe 14 Januari 2024, baada ya Silaa ambaye ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, alipowatembelea wananchi hao kwa ajili ya kusikiliza changamoto zao.
Mlezi wa kikundi cha madereva wa pikipiki (bodaboda), Bihimba Mpaya, alimohiji Silaa kwa nini hajatelekeza ahadi yake ya kuhakikisha barabara ya Banana-Kitunda-Kivule-Msongola, inakarabatiwa ili kuwoandolewa adha ya usafiri wananchi wake.
“Kuhusu barabara umeshaongea sana, ni mbovu wazazi wanazalia njiani kwa ajili ya barabara hii kuwa mbovu, baadhi ya wagonjwa wanafia njiani. Umeshakuja ukasema itafanyiwa matengeneza mpaka leo haijafanyiwa matengenezo na nina uhakika hili jambo halijakushinda kwa sababu una kampuni ya ujenzi greda liko mikononi mwako unaweza ukaikarabati hata kesho,” alisema Bihimba.
Katika hatua nyingine, Bihimba alimkabidhi Silaa orodha ya majina ya wafanyabiashara waliobomolewa vibanda vyao na kuharibiwa mali zao zenye thamani ya zaidi ya Sh. 13 milioni, ili awasaidie walipwe stahiki zao.
“Mwaka jana ilikuja bomoa bomoa ya mabanda wafanyabiashara walibomolewa mabanda yao kinyume cha sheria na mgambo na mali zao kuchukuliwa. Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo alikuja na akaahidi ataunda tume lakini hajaunda, tunakuomba ukasimamie wapate haki zao,”alisema Bihimba.
Kwa upande wa bodaboda, Bihimba alimuomba Silaa awachukulie hatua mgambo wanaowasumbua wasafirishaji hao abiri ili waache kuwatoza fedha kinyume cha sheria.
Akijibu maombo hayo, Silaa aliahidi kuyafanyia kazi huku akiwataka wananchi wampe muda.
Kuhusu ubovu wa barabara, Silaa ameahidi imeshafanyiwa usanifu na kwamba ukarabati wake utaanza Aprili 2024.
Leave a comment