IDADI ya vituo vya afya kuanzia 2017 hadi 2023, vimeongezeka kutoka 535 hadi kufikia 788, wakati zahanati zikiongezeka kutoka 4,127 hadi kufikia 5,646. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 28 Oktoba 2023 na Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mohammed Mchengerwa, katika hafla ya uzinduzi wa ripoti ya utafiti wa afya ya uzazi na mtoto na viashiria vya Malaria kwa 2022.
“Mwaka 2017 hadi 2013 Zanahati zimeongezeka kutoka 4127 hadi 5646, Vituo vya afya vilivyosajiliwa na kuanza kutoa huduma kutoka 535 hadi 788, vituo vya upasuaji kutoka 115 hadi 537 na jumla ya hospitali mpya zilizojengwa ni 119 na 18 zimekarabatiwa,” amesema Mchengerwa.
Katika hatua nyingine, Mchengerwa amesema kuanzia 2021 hadi 2023, TAMISEMI imetumia zaidi ya Sh. 194 bilioni, kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya afya na upatikanaji wa vifaa tiba na ujenzi wa majengo mbalimbali na ununuzi wa mitambo ya kuongeza hewa.
Aidha, Mchengerwa ameagiza wakuu wa mikoa kuhakikisha vituo vya afya vilivyokamilika ujenzi wake, kuanza kazi mara moja.
Leave a comment