Visima 27 vya maji kati ya 34 vilivyopimwa katika wilaya za Kahama na Kishapu mkoani Shinyanga vimebainika kuwa na vimelea vya ugonjwa wa kipindupindu. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hayo yamebainishwa leo Jumatano na Meneja wa Ubora wa Maabara ya Maji Mkoa wa Shinyanga, Marco Kayanda ambapo amesema kati ya visima 34 vilivyopimwa, visima 22 vilikuwa vya Manispaa ya Kahama ambako sampuli 18 zimekutwa na vimelea vya ugonjwa huo.
‘’Visiwa 12 vilivyopimwa vilikuwa vya Wilaya ya Kishapu; visima tisa vimebainika kuwa na vimelea vya Ugonjwa wa Kipindupindu,’’ amesema Kayanda.
Amesema hatua kadhaa tayari zimechukuliwa ikiwamo kunyunyiza dawa ya kuua vimelea katika visima vyote na kuhakikisha maji yake yanakuwa salama.
Naye Meneja wa Wakala wa Maji Vijijini Mkoa wa Shinyanga (Ruwasa), Julieth Payovela amesema uchunguzi wa awali eneo la Mji Mdogo Kagongwa umebaini kuwa visima vingi vimechimbwa jirani na vyoo.
“Wananchi wengi wanachimba visima bila kuzingatia kanuni na taratibu; baadhi wamechimba na kujenga visima ndani ya mita 10 kutoka kwenye vyoo tofauti na kanuni inayoelekeza uchimbaji na ujenzi wa kisima kufanyika umbali wa kuanzia mita 60 kutoka kwenye vyoo,’’ amesema Julieth.
Leave a comment