NGOME ya Vijana ya Chama cha ACT-Wazalendo, imetoa mapendekezo sita yatakayowezesha upatikanaji wa tume huru ya uchaguzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Mapendekezo hayo yalitolewa jana Jumatano, tarehe 9 Machi 2022 na Naibu Katibu wa Habari, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma wa ngome hiyo, Anthony Ishika akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam.
Miongoni mwa mapendekezo yaliyotajwa na Ishika ni kuandikwa upya kwa sheria na kanuni za uchaguzi, ili kupata tume hiyo.
“Kuandikwe upya sheria na kanuni za uchaguzi ili kupata tume huru, ambayo Itaajiri watendaji wake, sio mfumo wa sasa ambao wasimamizi wanakua makada wa chama tawala,” amesema Ishika.
Ishika amesema pendekezo la pili ni, maoni ya wananchi yaliyomo katika Rasimu ya Katiba ya Waziri Mkuu Mstaafu, Joseph Warioba, yachukuliwe kwa ajili ya kuanzia tume hiyo.
“Pendekezo la tatu, kuwe na kamati itakayoteua mwenyekiti, makamu mwenyekiti na wajumbe wa tume huru ya uchaguzi. Kamati hiyo izingatie ushirikishwaji wa vyama vyote, wadau na taasisi mbalimbali, ili kuleta usawa wa maamuzi,” amesema Ishika.
Ishika amesema pendekezo lingine la ngome hiyo, kamati hiyo izingatie usawa wa muungano kisheria, na iongozwe na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na makamu mwenyekiti awe Jaji Mkuu wa Zanzibar.
“Wajumbe wawe Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), ateuliwe mtu mmoja na mkuu wa shughuli za serikali bungeni, Ateuliwe mtu Mmoja na kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni,” amesema Ishika na kuongeza:
“Kama sivyo Chombo kinachojumuisha vyama vyenye wabunge Bungeni, Asasi za Kitaifa za Sheria na Haki za Binadamu Tanzania Bara mmoja na Mwingine Zanzibar. Uteuzi huo lazima uhusishe wanawake na Vijana.”
Leave a comment