KICHAPO cha goli 3 -1 ilichopokea Klabu ya PSG kutoka kwa wababe Real Madrid kimemuweka matatani kocha Mauricio Pochettino baada ya ndoto ya kutwaa kombe la Klabu Bingwa Ulaya (UEFA Champions League) kuyeyuka.
Hatua hiyo imekuja baada ya jana tarehe 9 Machi, 2022 Real Madrid kuwafungasha virago matajiri hao wa Ufaransa katika hatua ya 16 bora. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea)
Wababe hao wa Uhispania waliondoka na ushindi wa jumla ya mabao 3-2 katika mchezo wao wa pili uliochezwa katika Uwanja wa Santiago Bernabeu baada ya mchezo wa kwanza PSG kushinda bao 1-0.
Bao la PSG lilipachikwa kimiani na Kylian Mbappe dakika ya 39 huku yale ya Real Madrid yakipachikwa na mkongwe asiyeishiwa makali Karim Benzema dakika 61,76 na 78.
Benzema mwenye umri wa miaka 34, sasa amefunga hat trick tatu na kufikisha jumla ya mabao 105 katika michuano hiyo.
Aidha, kitendo cha PSG kufungashwa virago katika michuano hiyo huku ikiwa na mastaa wanaong’ara duniani kama Mbape, Lionel Messi na Neymar Jr, kimedaiwa kumkasirisha Rais wa timu hiyo Nasser Al-Khelaifi na kueleza kuwa anatafakari hatua ya kuchukua.
Kwa mujibu wa gazeti la L’Equipe la nchini Ufaransa, sasa kocha huyo anatarajiwa kutupiwa virago muda wowote hasa ikizingatiwa lengo kubwa la PSG ni kutwaa taji hilo la Ulaya na si Ligi Kuu pekee.
Licha ya kuongozi Ligi Kuu Ufaransa kwa tofauti ya ponti 13, sasa inaelezwa kuwa Manchester United wanajipanga kumdaka kocha huyo iwapo atatimuliwa.
Leave a comment