SERIKALI kupitia wizara ya Maliasili na utalii imezitaka Taasisi zilizopo chini ya Wizara hiyo kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero katika kutatua changamoto ya tembo ambao wanasababisha madhara kwa wananchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).
Akizungumza leo Aprili 4,2024 mbele ya mamia ya Wakazi wa Vijiji vya Mangae, Doma na Mkata Wilayani Mvomero, wakati wa Operesheni ya kuyarudisha makundi ya Tembo Hifadhi ya Taifa ya Mikumi, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe.Dunstan Kitandula (Mb), amesema kwa kutumia helikopta makundi yenye jumla ya Tembo 45 waliokuwa kwenye maeneo ya makazi ya wananchi yamerejeshwa hifadhini katika zoezi linaloendelea kwa siku ya kesho.
Kitandula ameeleza zoezi la kuwarejesha tembo hifadhini ni jitihada za makusudi zilizofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kuwahakikishia usalama wananchi na uhifadhi endelevu nchini.
“Zoezi hili la kutumia Helikopta limetumia gharama kubwa, lakini licha ya ukubwa wa gharama hizi Serikali imejipanga kupunguza kero kwa wananchi wa maeneo haya ambao kadhia za wanyama hawa zimekuwa zikihatarisha usalama na mali zao,” alisema Kitandula.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Judith Nguli akimuwakilisha mkuu wa Mkoa wa Morogoro, ameipongeza Serikali kupitia Wizara ya Maliasi na Utalii kuwezesha zoezi la kuwaswaga Tembo kwa kutumia Helikopta kwani changamoto ya Tembo ni ya muda mrefu kwa wananchi
Kwa upande wake Mbunge wa Mvomero, Jonas Zeeland amesema uwezeshaji wa zoezi hilo ni faraja kwa wananchi kwani tembo wamekua wakileta uharibifu mkubwa wa mali na kuatarisha usalama wa Wananchi ambapo ameiomba Serikali kuendelea kuwasaidia kuepukana na changamoto hiyo.
“Naishukuru Serikali kusikia kilio cha wananchi na kuchukua hatua baada ya kuleta mapendekezo bungeni na kwa Waziri wa Maliasili na Utalii.”
Akielezea vifaa vya kujikinga na tembo vilivyokabidhiwa na Wizara kwa wananchi, Mkurugenzi wa Taasisi ya Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) Dk. Eblate Ernest Mjingo amesema Taasisi hiyo imeendelea kubuni mbinu mbadala za kutatua changamoto za migongano za kati ya binadamu na Wanyamapori nchini hususani tembo.
“Tafiti zimesaidia matumizi ya teknolojia katika kutatua migongano hiyo ikiwa ni pamoja na teknojia ya helkopta na mikanda ya visukuma mawimbi( GPS Coller),” alisema Dk. Mjingo.
Uzinduzi rasmi wa Operesheni hiyo umefanyika katika Kijiji cha Maenga Wilaya ya Mvomero na kuwajumuisha Viongozi wa Chama na Serikali na Viongozi wa kijamii wa Wilaya hiyo.
Leave a comment