TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Songwe imemnasa Eliam Fiabo anayedaiwa kuwa mkandarasi kwa tuhuma za kukusanya fedha kwa wananchi wa kijiji cha Shiwinga ili awaunganishie umeme jambo ambalo hakuwa na uwezo nalo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Songwe … (endelea).
Hatua hiyo imekuja baada ya Mkuu wa Mkoa huo, Omary Mgumba kuiagiza Takukuru kushughulikia madai ya wananchi wa kijiji hicho kilichopo kata ya Shiwinga, wilayani Songwe mkoani humo kwamba walichangishwa fedha ili waunganishiwe umeme jambo ambalo halikutekelezwa.
Akiwa katika ziara yake mkoani humo, wiki iliyopita, wananchi hao walidai kuwa walichangishwa fedha zaidi ya Sh milioni moja mwaka 2019 ili waunganishiwe umeme lakini wanashangaa hadi sasa hawajapata nishati hiyo.
Aidha, akizungumzia hatua walizochukua mapema wiki hii, Ofisa wa Takukuru mkoa wa Songwe, Priscilla Mbena amesema walimkamata mtuhumiwa huyo Eliam Fiabo aliyekusanya fedha hizo na kisha kumhoji.
Amesema mtuhumiwa huyo alikiri kutenda kosa hilo na alitakiwa kuwarudishia wanakijiji hao pesa zao.
Ofisa huyo wa Takukuru akiwa ameongozana na Diwani wa Kata ya Shiwinga, Isabela Mbaya (CCM) walifika kijijini hapo na kuonana na wananchi waliotapeliwa fedha hizo.
“Wale wote waliotupatia risiti zao zilizoonyesha kufanya malipo kwa huyo mkandarasi napenda kuwaambiwa tumefanikiwa kuokoa fedha zenu na mtuhumiwa amerejesha hivyo tunawarudishia hela zenu hapa mbele ya viongozi wenu wa Kijiji na diwani wenu”- alisema Priscilla Mbena
Kwa upande wa Diwani wa kata hiyo, Isabella Mbaya amemshukuru Mkuu wa Mkoa huo kwa kusikiliza kero za kata yake kisha kuwapa maagizo ambayo ndani ya muda mfupi yametelekeza.
Pia amewashukuru Takukuru Songwe kwa kuonesha jinsi gani walivyo makini kutatua matatizo ya wananchi.
Jumla ya fedha iliyookolewa na Takukuru ni shilingi milioni 1,180,000 ambazo walitapeliwa mwaka 2019 na mkandarasi huyo anayefahamika kwa jina la Eliam Fiyabo.
Leave a comment