Sudan imemrejesha nyumbani balozi wake nchini Kenya kufuatia ziara na kikao kati ya Rais wa Kenya, William Ruto na Kamanda wa kikosi cha RSF, Mohamed Hamdan Dagalo, kinachopingana na jeshi la Sudan chini ya Abdel Fattah al-Burhan. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa …(endelea).
Kwenye taarifa iliyochapishwa jana Alhamisi na shirika rasmi la habari la SUNA, Kaimu waziri wa mambo ya nje wa Sudan, Ali al-Sadiq, balozi huyo ameamriwa kurejea nyumbani ili kufanya majadiliano zaidi kufuatia mapokezi ya hasimu wao nchini Kenya.
Kwa mtazamo wake, matokeo ya majadiliano ndiyo yatakayoamua hatima ya uhusiano kati ya Sudan na Kenya.
Kamanda wa kikosi cha Rapid Support Forces, RSF, Mohamed Hamdan Dagalo, alifanya kikao na Rais William Ruto siku ya Jumatano.
Hamdan ameyazuru kwa mara ya kwanza mataifa kadhaa ya Afrika tangu vita kuzuka Aprili mwaka uliopita.
Kwa upande wake Rais Ruto alichapisha picha za mkutano wao kwenye mtandao wa kijamii wa X na kuelezea kuwa amepokea vizuri nia ya RSF na Dagalo ya kutaka kumaliza mapigano ya Sudan kupitia mazungumzo.
Kabla ya kuwasili Nairobi, Kamanda Hamdan Dagalo akiwa Sudan aliafiki kuwa wako tayari kwa mazungumzo ya amani walipotiliana saini makubaliano ya amani na muungano wa vyama vya kiraia.
“Tunaunyosha mkono wa amani. Kama wanataka amani, tunawakaraibisha. Hakuna kitakachotuondoa Khartoum isipokuwa amani,” kamanda huyo alikaririwa akisema hivi karibuni.
Juhudi za kikanda za upatanishi na kusitisha mapigano bado hazijafua dafu. Ifahamike kuwa kamanda Hamdan Dagalo ameshayazuru mataifa ya Uganda, Ethiopia na Djibouti.
Duru zinaeleza kuwa kwa sasa amekutana na rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa mjini Pretoria.
Leave a comment