SHURA ya Maimamu Tanzania, imeitaka Serikali kuchukua hatua dhidi ya watu wanaofanya au kuhamasisha vitendo vya mapenzi ya jinsia moja, ili kulinda maadili na tamaduni za nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumamosi, tarehe 22 Aprili 2023 na Katibu wa Shura ya Maimamu Tanzania, akisoma waraka wa Idd Elfitry wa taasisi hiyo.
Kupitia waraka huo, Sheikh Ponda amedai kitendo cha Serikali kutotoa msimamo thabiti pale matukio hayo yanapoibuliwa ndani ya jamii, kinaweza sababisha matukio hayo kushamiri zaidi.
Sheikh Ponda ametolea mfano shule moja iliyoko mkoani Kilimanjaro ambayo ilikutwa na vitabu vinavyofundisha mapenzi ya jinsia moja, akisema ilipaswa kuifungia badala ya kuiacha iendelee kufundisha watoto.
Aidha, Sheikh Ponda ameishauri Serikali kufanya ufuatiliaji wa kina shughuli zinazofanywa na asasi za kiraia pamoja na mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO’s), akidai baadhi yake hutumika kufadhili na kuhamasisha vitendo hivyo.
Akisoma waraka huo, Sheikh Ponda ameishauri Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria kusitisha nia yake ya kuwasilisha muswada wa sheria ya ndoa bungeni jijini Dodoma, wenye lengo la kuweka sharti la mtu kutofunga ndoa chini ya umri wa miaka 18.
Sheikh Ponda amedai kuwa, Sheria hiyo ikipitishwa itahamasisha baadhi ya watu watakaobalehe kabla ya umri huo, kushawishika kufanya mapenzi ya jinsia moja hasa ushoga, kwa kuwa watakosa fursa ya kufunga ndoa mapema.
“Binti aliyevunja ungo anayetaka kufunga ndoa akizuiliwa, anaumia na kuathirika sana kimaumbie. Kijana huyo ikiwa ataogopa aibu ya umalaya ni rahisi kwake kukubaliana na msichana
mwenzie kukidhi mahitaji yao kwa kusagana.
Vile vile mvulana balehe anayetaka kufunga ndoa akizuiliwa anaumia na kuathirika sana. Naye pia ikiwa ataogopa aibu ya umalaya ni rahisi kikubaliana na mvulana mwenzie kukidhi mahitaji yao kwa ushoga,” amesema Sheikh Ponda.
Katika hatua nyingine, Sheikh Ponda amesema Shura hiyo inaishauri Serikali kupeleka muswada wa Sheria ya kuhamasisha ba kulinda ndoa za kidini bungeni, ili kuwe na ndoa zinazojenga jamii yenye maadili.
Leave a comment